https://monetag.com/?ref_id=TTIb Bilioni 12 kufikisha maji Magu | Muungwana BLOG

Bilioni 12 kufikisha maji Magu

JUMLA ya Sh. 12 Bilioni zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza mradi wa maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Magu mkoani Mwanza ili kutatua tatizo hilo, anaandika Moses Mseti.

Hayo yamebainishwa leo na Bonevature Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Magu wakati akizungumza na mtandao huu kuhusu tatizo la maji katika wilaya hiyo.

Kiswaga amesema kuwa, tatizo hilo katika jimbo lake limedumu kwa kipindi kirefu sasa, hivyo suala hilo linatarajiwa kushughulikiwa kwa ukaribu na kuwasaidia wananchi kuondokana na adha ya maji.

Amesema kuwa, hivi sasa wapo katika hatua za upembuzi yakinifu chini ya Kampuni ya Cowi ambayo inakaribia kukamilisha kazi hiyo wezi huu na baadaye kutangazwa tenda ili kuanza mradi huo.

“Tatizo maji katika Wilaya ya Magu bado ni kubwa sana na hivi sasa ndio tupo katika hatua za upembuzi yakinifu,” amesema Kiswaga.

Kiswaga amesema kuwa, tatizo la maji katika wilaya hiyo katika uongozi wake litakuwa historia kwani amejipanga kulishughulikia kwa ukaribu zaidi.

Pia amesema, Wilaya ya Magu pamoja na kukabiliwa na tatizo la maji pia kuna tatizo la barabara ambazo alidai zimeharibika na zinahitaji kufanyiwa matengenezo ya uhakika ili kuzinusuru.