https://monetag.com/?ref_id=TTIb Wamachinga Manispaa ya Ilala Waiomba Serikali Kuwaongezea Muda | Muungwana BLOG

Wamachinga Manispaa ya Ilala Waiomba Serikali Kuwaongezea Muda

Wamachinga wa manispaa ya Ilala jijini dar es salaam wameiomba serikali kuwaongezea muda wa kuhamia katika maeneo yaliyotengwa na manispaa hiyo kutokana na baadhi ya masoko kutokamilika kwa miundombinu ikiwemo vyoo na maji huku pia idadi iliyotolewa ikitajwa kuwa ndogo ukilinganisha na idadi yao halisi.

Akizungumza na channel ten mwenyekiti wa machinga Ilala Steven Lusinde amesema kuwa kimsingi wao hawapingi amri ya serikali ya kuhamia katika masoko hayo wala hawahitaji nguvu kutumika katika kuwaondoa bali wanaiomba serikali iwape muda zaidi wa kukaa na wanachama wao kwa ajili ya kuwapatia elimu kwani awali walikuwa na ushirikiano mzuri na mkurugenzi wa jiji ambaye aliwataka kuwatambua wamachniga wote katika manispaa yake ambao kwa idadi yake wamedai kuwa hawawezi kutosheleza katika maeneo hayo kwani kariakoo peke ina wamachinga zaidi ya elfu tatu.

Aidha mwenyekiti huyo amelalamikia kuachwa kwa jengo la machinga complex katika masoko yaliyoainishwa na mkurugenzi wa Ilala wakati wao wanatambua kuwa jengo hilo lilijengwa kwa ajili yao lakini limehodhiwa na watu wasiostahili huku wamachinga wakipata misukosuko barabarani wanakupanga bidhaa zao.

Jana mkurugenzi wa manispaa ya Ilala Isaya Mngurumi alitoa siku mbili kwa wamachinga kuondoka katika mitaa ya kariakoo na kando kando ya barabara za manispaa hiyo na kuhamia katika maeneo yalitengwa ikiwemo Kigogo fresh, kivule, tabata muslim na ukonga magereza.