Heshima kwa ngoma yangu na Alikiba - Bonge la Nyau

Msanii Bonge la Nyau ambaye kwa sasa anafanya vizuri na wimbo wake wa 'Aza' amefunguka na kusema katika ngoma zake zote alizofanya mpaka sasa ameiheshimu sana kazi aliyoifanya na msanii Alikiba.

Akiwa kwenye kipindi cha 5Selekt, Bonge la Nyau amedai kuwa anaiheshimu sana kazi yake 'Uaminifu' ambayo alishirikiana na msanii Alikiba na kusema wimbo ule ndiyo umeweza kumtambulisha vyema kwa watanzania na uliweza kuwafikia watu wengi zaidi na wengi waliupenda zaidi.

"Nimefanya nyimbo nyingi lakini kiukweli mpaka sasa wimbo niliofanya na Alikiba nauheshimu sana moja kwa sababu ni wimbo ambao umeangaliwa sana 'Youtube' kuliko nyimbo zangu nyingine, lakini pia ni wimbo ambao nikipanda stejini kuimba naimba na mashabiki mwanzo mwisho, sababu wanaifahamu vyema hivyo wimbo ule kwangu ni mkubwa sana". Alisema Bonge la nyau
Mbali na hilo Bonge la Nyau amedai kuwa yeye hategemei skendo katika kufanya kazi zake bali yeye anategemea sana kufanya kazi nzuri ambazo zinaishi ndiyo maana hata leo ukichukua kazi zake na kusikiliza utagundua ni kazi ambazo zinaishi.