Makundi yayumbisha CCM

KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) jijini Arusha, Medest Meikoki amesema kuyumba kwa chama hicho katika Jiji la Arusha na kusababisha upinzani kuongoza kutokana na makundi yaliyopo ndani ya chama hicho.

Akizungumza mjini hapa jana, Meikoki alisema aliamua kustaafu siasa baada ya kusulubiwa na makundi hayo ambayo kwa kiasi kikubwa yalikuwa na nguvu katika miaka ya 2000.

Alisema katika jiji hili kulikuwa na makundi mawili ya G7 na G13 ambayo yalikuwa na nguvu katika miaka hiyo.

Kada huyo, alisema bado baadhi ya wana CCM waliojeruhiwa na makundi hayo wana hasira dhidi ya chama chao na kuamua kukaa pembeni na kuacha wenye pesa wafanye watakavyo, lakini waliapa chama hakitachukua jimbo hilo kamwe.

Alisema hatua za ziada zinatakiwa kuchukuliwa na viongozi wa juu wa CCM wa kuwarudisha kundini waliojeruhiwa na makundi hayo bila ya sababu za msingi vinginevyo, upinzani utaendelea kuongoza.

Kada huyo aliendelea kusema kuwa makundi ya kisiasa ya G7 na G13 ndiyo yamekivuruga chama na kuifikisha siasa ya Arusha kuwa taabani kwani waliokuwa wakichaguliwa walikuwa ni viongozi wasiokuwa na sifa za kuongoza chama hicho.

Alisema, kundi la G7 lilikuwa kundi lenye uwezo mkubwa wa kifedha ambapo wafanyabiashara wakubwa wa Arusha, walikuwa katika kundi hilo na walikuwa wakiamua wanavyotaka na ukipingana nao unang’olewa.

Kada huyo alisema, kundi la G13 lilikuwa kundi la wanasiasa wenye kujua siasa za Arusha na nchi kwa ujumla na walikuwa wapambanaji lakini walikuwa ni watu wa kawaida tu wasiokuwa na fedha, lakini wenye mikakati ya kutaka chama kishike hatamu.

Alisema yeye aliwahi kushughulikiwa mwaka 2000 ndani ya chama na kundi la G7 kwani katika kura za maoni za ndani ya chama, alishinda lakini kundi hilo halikuridhika na likaamua kumtoa mwanaCCM na kumsimamisha upande wa Chama cha Tanzania Labour (TLP) ili kupambana naye kwenye udiwani wa kata ya Darajambili.

Kada huyo alisema kundi hilo lilifanikiwa, kwani TLP ilishinda katika kiti cha udiwani katika kata hiyo na yeye kuanguka vibaya ingawa awali alishinda kwa kishindo katika kura za maoni ndani ya chama

Alisema baada ya kushughulikiwa mwaka 2000 aliamua kujikita katika kushauri badala ya kugombea na alipoamua kuingia tena kwenye siasa mwaka 2005, alishughulikiwa tena na akaamua kustaafu na kubakia kuwa mshauri hadi sasa.