Mwanariadha aliyepinga serikali ya Ethiopia

 Mwanariadha wa Ethiopia Feyisa Lilesa ametajwa kama mwanariadha mkakamavu kwenye michezo ya olimpiki ya mwaka huu iliyokamilika mjini Rio , Brazil baada ya kuonyesha ishara za upinzani dhidi ya serikali.

Lilesa amesema jamaa zake wamekamatwa na maafisa wa usalama wa Ethiopia.

Mwanariadha huyo amesema anahofia anaweza kukamatwa iwapo atarudi nchini humo na kwa hivi sasa atatafuta makao Ulaya.

Serikali imepuzilia madai hayo na kusisitiza iwapo atarudi nchini humo atapokelewa kama shujaa kwa kuipeperusha bendera ya taifa hilo kwenye olimpiki.

Upinzani wake dhidi ya serikali, ni kama alivyoutaja kama 'mauaji ya watu wake'.

Watu kwenye mitandao ya kijamii walimuunga mkono mwanariadha huyo kwa hatua aliyoichukua.

Lakini kituo cha televisheni cha serikali hakijaonyesha picha za mwanariadha huyo za ushindi au hata taarifa aliyoitoa kwa vyombo vya habari.

Maelfu ya wanaopinga serikali kutoka kwa jamii hizo kubwa za Oroma na Amhara wamekuwa wakiandamana kwa wiki kadhaa wakitaka mageuzi ya jinsi serikali hiyo inavyoendesha shuguli zake.

Kundi la kutetea haki za kibinadamu limesema zaidi ya watu 100 wameuawa kwa wiki zilizopita tangu maandamano mapya kuanza .

Serikali imepinga idadi hiyo.