Polisi Rukwa wamzuia Lowassa kuingia

Aliyekuwa mgombea wa Urais kupitia Chadema, Edward Lowassa 

Mbeya. Msafara wa aliyekuwa mgombea wa Urais kupitia Chadema, Edward Lowassa umekwama kwenda Mikoa ya Rukwa na Katavi  baada ya polisi kuuzuia kwa hofu kwamba unaweza kuingilia ziara ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa anayetembelea mikoa hiyo.

Lowassa ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema alianzia ziara yake  mkoani hapa tangu Agosti 21 na juzi alifanya vikao vya ndani katika majimbo yanayoshikiliwa na wabunge wa chama chake  mkoani  Songwe wakati leo asubuhi alitarajiwa kwenda Katavi na Rukwa.

Katika Mikoa ya Rukwa na Katavi alitarajiwa kufanya mikutano ya ndani Majimbo ya  Nkasi Kaskazini na Kusini na Sumbawanga.

Katibu wa Chadema Kanda ya Nyanda za Juu Kusini wanayoiita ‘Kanda ya Nyasa’, Frank Mwaisumbe  alisema  kwamba polisi walimpigia simu Lowassa juzi saa 1.00 jioni akiwa Tunduma  wakimtaka aahirishe ziara yake Mkoa wa Rukwa.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Rukwa, Gorge Kyando alipoulizwa  kwa njia ya simu alisema waliwashauri viongozi wa Chadema wapange siku nyingine ya ziara kwa sababu  mkoa ulikuwa na ugeni mkubwa.