https://monetag.com/?ref_id=TTIb Watanzania 56 watekwa na kuuawa na askari wanaodhaniwa kuwa wa nchi jirani. | Muungwana BLOG

Watanzania 56 watekwa na kuuawa na askari wanaodhaniwa kuwa wa nchi jirani.

Zaidi ya watanzania 56 katika vijiji vya Chamchuzi na Buguluka vilivyoko katika kata ya Bwelanyange iliyoko wilayani Karagwe mkoani Kagera waliokuwa wakijihusisha na shughuli za uvuvi ndani ya mto Kagera na ziwa hiema wanadaiwa kutekwa na kuuawa kikatili na watu wanaodhaniwa kuwa ni askari wa nchi jirani Rwanda ambao mara kwa mara hufanya doria ndani ya mto huo na ziwa hilo.

Vitendo vya watanzania kutekwa na kuuwawa kikatili vimeshtua mkuu wa wilaya ya Karagwe Godfrey Muheruka anayelazimika kufanya ziara ya kutembelea mwalo wa Rukombe ambao hutumiwa na wananchi wa vijiji vya Chamchuzi na Buguluka na baadae kukutana na wananchi wa vijiji hivyo viwili miongoni mwao wakiwemo wajane 59 ambao wanaume wao wanasadikiwa kuuwawa, baadhi ya watanzania walionusurika kifo wenye majeraha mbalimbali ya risasi na mtanzania aliyekombolewa hivi karibuni toka nchini Rwanda ambao wametoa shuhuda mbalimbali.

Afisa mtendaji wa kata ya Bwelanyange Nicolaus Lubambala kwenye taarifa yake iliyosomwa na Godwin Mbeikya ambaye mratibu elimu kata ya Bwelanyange ameeleza kuwa matukio ya watanzania kuuwawa yamekuwa yakiongezeka kila kunapokucha, kufuatia matukio hayo mkuu wa wilaya ya Karagwe Godfrey Muheruka amepiga marufuku shughuli za uvuvi ndani ya mto Kagera na ziwa hiema hadi ufumbuzi wa tatizo hilo utakapopatikana.

Hivi karibuni watanzania 9 katika wilaya ya Kyelwa waliokuwa wakifanya shughuli za uvuvi ndani ya mto Kagera waliuwawa na watu wanaodhaniwa askari wa nchi jirani ya Rwanda hali ambayo ilimsikitisha waziri wa mambo ya ndani Mwigulu Nchemba aliyepata taarifa hiyo wakati akiwa mkoani Kagera.