Bomba la mafuta lalipuliwa Nigeria

Kumwagika kwa mafuta kumechafua mazingira nchini Nigeria

Kundi la waasi katika eneo lenye utajiri wa mafuta nchini Nigeria linasema kuwa limelipua bomba la mafuta kama sehemu ya kampeni yenye kichwa "tunamiliki ardhi zetu."

Afisa wa idara ya ujasusi nchini Nigeria, aliliambia shirika la habari la AFP kuwa bomba hilo lililipuliwa na kundi la waasi

Bomba hilo liko chini ya usimamizi wa kampuni ya Nigeria Petroleum Development , sehemu ya kampuni ya serikali ya Nigeria Petroleum Corporation.

Eneo hilo lenye utajiri wa mafuta la kusini mwa nchi, limeshuhudia mashambulizi tangu Rais Muhammadu Buhari ambaye anatoka kaskazizi aingie madarakani mwaka uliopita.

Waasi wanataka wapewe mgao wa utajiri wa mafuta na pesa kutoka kwa mauzo ya mafuta kutumiwa kupambana na umaskini eneo hilo. Aidha wametaka kumalizika kwa uchafuzi unaosababishwa na sekta ya mafuta.