Ozil: Iwobi ni mchanganyiko wa Okocha na Edgar Davids

Mesut Ozil amemwaga sifa kedekede kwa kiungo mshambuliaji mwenza wa Arsenal Alex Iwobi n kusema kuwa aina ya uchezaji wake ni mchanganyiko wa Jay-Jay Okocha na Edgar Davids.

Iwobi, 20, amechezea Arsenal michezo sita mpaka sasa msimu huu na tayari ametoa pasi tatu za magoli, hivyo Ozil ameshindwa kuzuia hisia zake na kuweka wazi ubora wa kinda huyo kwa maana ya nguvu na matumizi makubwa ya akili.

“Ananikumbusha enzi za mjomba wake, Jay-Jay Okocha,” Ozil alisema. “Ni aina ya wachezaji niliopenda sana kuwaangalia.

“Alex ananikumbusha vionjo alikuwa navyo Okocha na Edgar Davids. Ni makini anapokuwa na mpira, pia mzuri linapokuja suala la kulinda, na mbele ya goli ndio usiseme.

“Kiukweli anaendelea vizuri na kama ataendelea kama ambavyo amekuwa akicheza, basi atafanya mabo makubwa sana.

“Meneja anajua hasa namna gani alivyo mzuri na niseme tu namtakia kila la heri katika safari yake ya maisha ya soka.”