Wastara Apata Ubalozi wa Simu za KZG, Atalipwa Mil 400 Kwa Mwaka

 Meneja wa Wastara, Bond Suleiman, akiwakaribisha wageni waalikwa na waandishi wa habari (hawapo pichani).

 Meneja wa KZG, Raymond Kalikawe (kushoto) akitoa ufafanuzi kuhusu kampuni hiyo.

 Wastara (kulia) akielezea jinsi alivyofurahia ubalozi huo.

 Wastara (katikati) akisaini mkataba huo.

 Wakibadilishana mkataba na meneja wa KZG, Kalikawe.

 Meza kuu wakionyesha aina za simu hizo.

Wakikata keki ambayo ni maalum kwa ajili ya siku ya kuzaliwa ya Wastara.

Staa wa filamu Bongo, Wastara Juma amepata shavu la kuwa balozi wa Kampuni ya simu ya mkononi ya KZG ambapo leo amekabidhiwa na kusainishwa mkataba rasmi.

Akizungumza katika tukio la kusaini makubaliano ya kuwa balozi wa kampuni hiyo  lililofanyika katika ukumbi wa De Mag Hotel iliyopo Mwananyamala, Dar,  Wastara alisema amefurahi sana kupata shavu hilo kwani kujituma kwake katika biashara ndiko kulikompatia bahati hiyo.

Aliendelea kusema kwamba atahakikisha anafanya vizuri katika ubalozi huo ambao kwa mwaka unampatia shilingi milioni mia nne kutegemea na jinsi kampuni hiyo inavyouza bidhaa zake hizo kwani imempa heshima kubwa ambayo hakuitarajia.

“Nina furaha sana kuwa balozi wa KZG, hii imetokana na kujituma kwangu kwani ninafanya biashara nami ni mwanamke ambaye ninajitambua na najua ninachokifanya, naishukuru kampuni hii kwa kuniona hivyo, naomba mashabiki zangu waniunge mkono,” alisema Wastara.

Katika tukio hilo pia kampuni hiyo ilimzawadia keki Wastara ikiwa ni zawadi ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake kwani ilikuwa jana, hivyo kutokana na nafasi hiyo wakaona ni vyema wampe zawadi hiyo iliyokuwa imechorwa aina mojawapo ya simu za KZG.