Samatta amehoji kwa nini Farid bado yupo Tanzania?

Ni ndoto ya kila mtanzania mpenda maendeleo ya soka la Bongo kuona wachezaji wengi wanatoka kwenda kucheza soka la kulipwa nje ya Tanzania kwa ajili ya maendeleo ya soka letu hususan timu ya taifa ‘Taifa Stars’.

Nahodha wa timu ya taifa ya Tanzania Mbwana Samatta ambaye kwa sasa anacheza soka la kulipwa barani Ulaya, amehoji mustakabali wa Farid Musa kucheaza soka Ulaya baada ya winger huyo wa Azam kufuzu majaribio yake lakini siku zinazidi kuyoyoma bado anaendelea kuwepo Tanzania huku akiwa hachezi.

Katikati ya mwezi April mwaka huu Farid alikwenda Hispania kufanya majaribio kwenye klabu ya Tenerife na akafanikiwa kufuzu majaribio hayo huku klabu hiyo ikionesha nia ya kutaka saini ya kinda huyo mtanzania.

Lakini tangu aliporejea nchini toka Hispania bado hajaondoka huku akiwa hachezji mechi za ligi kuu Tanzania bara kitu ambacho kimefanya Samatta kuhoji kama kuna kitu kipo nyuma ya pazia kuhusu Farid kuendelea kuwepo Bongo.

“Asalam aleikhum? Niliposikia farid anaenda Spain kwa majaribio nilipata furaha sana kwa kuwa niliamini kwa kipaji alichonacho asingeweshindwa majaribio ktk club ile aliyokuwa anakwenda na ndivyo ilivyokuwa furaha iliongezeka baada ya kusikia azam wamemruhusu kwenda kuanza maisha ayo mapya ya soka Ulaya,”ameandika Samatta kupitia ukurasa wake wa Instagram.

“Kwa nini niwe na furaha kwa sababu naamini maendeleo ya timu yetu ya taifa yatapiga hatua kwa haraka tukiwa na wachezaj wengi wanaocheza soka la kulipwa nje ya tanzania, (imani yangu) lakini kadri siku zinavyokwenda nimekuwa simsikii Farid akiwa ktk club yake mpya na habari zilizopo ni kuwa bado yuko Tanzania, je ni kwa nini bado yupo Tanzania wakati kila kitu kilishakwisha nani ana jibu la swali hili? Tafadhali kuna nini nyuma ya pazia?”

Kwa mujibu wa C.E.O wa Azam FC siku ambayo alimtambulisha Abdul Mohamed kama General Manager wa klabu hiyo alisema, kila kitu kimeshakamili na wao (Azam FC) wameshatuma ITC ya Farid kwenda Tenerife lakini kinachomkwamisha Faridi ni kibali cha kufanya kazi nchini Hispania ambacho kinashughulikiwa na klabu yake mpya na sio Azam FC.