Masogange apelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali

Dar es Salaam. Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu Dar es Salaam, Simon Sirro amesema mtuhumiwa Agness Gerald, maarufu Masogange amepelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kuchukua vipimo vya damu ili kubaini kama anatumia dawa za kulevya.

Masogange ambaye ni mrembo maarufu anayetamba katika video za wasanii mbalimbali wa bongo fleva alikamatwa na polisi juzi.

Kamishna Sirro amewaambia wanahabari leo kuwa Masogange amepelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali na kwamba majibu yakipatikana kesho atafikishwa mahakamani

"Tunamchunguza Masogange katika mambo matatu ili kujua kama anauza , anatumia au anasafirisha dawa za kulevya, " amesema Kamishna Sirro.

Katika hatua nyingine, Kamishna Sirro amesema watuhumiwa 349 wamekamatwa kwenye operesheni ya kupambana na dawa za kulevya iliyoanza Februari Mosi mwaka huu.