Ray C: Nahitaji mpenzi wa miaka 60

Mtangazaji wa kipindi cha NIRVANA Deogratius Kithama akiwa na msanii Ray C.

Msanii Ray C amesema  sasa hana muda tena wa kuhangaika na vijana katika mapenzi na kudai anatafuta mzee wa miaka 60 atulie naye.

Ray C amesema hayo jana kupitia kipindi cha NIRVANA wakati akihojiwa na Deogratius Kithama na kusema sasa anatafuta mzee kuanzia miaka 60 ndiyo anaweza kuwa naye kwenye mahusiano na kusema muda wa kucheza na vijana kwake umeshapita.

"Nimeshakuwa sana katika mahusiano na vijana naona hakuna jipya sasa nimeamua kutoka huko na kutafuta mtu mzima angalau miaka hamsini hivi, tena hata huyo naona bado kijana bora awe na miaka sitini hivi nitulie naye, hawa vijana wameshanichosha mimi" alisema Ray C

Mbali na hilo Ray C alizungumzia juu ya jaribio lake la miaka ya nyuma kutaka kubadili kifua chake na kusema ni kweli alitaka kufanya hivyo kwani anaamini kila binadamu kuna kitu anaweza kutaka kukifanya vile ambavyo yeye anapenda kiwe, japo jambo hilo hakuweza kulifanya.