Waziri Mhagama atoa siku 30 kwa Waajiri

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu, Bunge, Kazi,Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu, ametoa siku 30 kwa waajiri wote nchini ambao hawajasajili, kujisajili katika mfuko wa fidia kwa wafanyakazi (WCF) na kutoa michango kwa wakati.

Mh. Mhagama ametoa agizo hilo leo jijini Mbeya wakati wa ukaguzi wa kushtukiza jijini humo na kuwabaini waajiri ambao bado hawajatekeleza Sheria ya fidia kwa Wafanyakazi Sura 263 Marejeo ya Mwaka 2015 kifungu cha 5, ambayo inawataka waajiri wote kutoka sekta ya Umma na binafsi Tanzania Bara kujisajili kwenye mfuko huo.

Mhagama amefafanua kwamba, mwajiri ambaye hajajisajili kwenye mfuko, anaweza kufikishwa mahakamani na adhabu ni pamoja na kutozwa faini ya kiasi cha fedha kisichozidi shilingi milioni 50 au kifungo kisichozidi miaka 5 jela au vyote kwa pamoja,
Katika ziara hiyo ya ukaguzi wa kushtukiza Mh. Mhagama alifuatana na Mkurugenzi wa Huduma za Tiba na Tathmini wa Mfuko wa fidia kwa wafanyakazi, Dk. Abdulsalaam Omar, na aliikagua hospitali ya K’s iliyoko eneo la Mafyati na Shule ya Sekondari ya Saint Aggrey iliyoko Uyole na kubaini kuwa taasisi hizo hazijajisajili katika mfuko.