Mnangagwa aapishwa kuwa Rais wa Zimbabwe

Rais mpya wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa ameapa mchana huu na hivyo kuhitimisha miaka 37 ya utawala wa Robert Mugabe aliyetangaza kujiuzulu tangu Jumanne iliyopita.

Mamia ya wananchi wa Zimbabwe wamefurika katika uwanja wa Harare kushuhudia sherehe hizo ambazo pia zimehudhuriwa na marais wa mataifa matatu.

Kelele za vivijo na nderemo zimesikika wakati Mnangagwa akikamilisha kiapo chake. Mitaani kumekuwa na hali ya shamra shamra za tukio hilo lililokuwa likisubiriwa na wengi.