Waziri mkuu atoa agizo la mwezi mmoja kwa Ofisa Ardhi

Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa, ametoa mwezi mmoja kwa Ofisa Ardhi wa wilaya ya Namtumbo Bw. Maurus Yera kuhakikisha anatafuta ardhi ya kuwafidia wakazi wa kijiji cha Lwinga wilayani humo.


Waziri Mkuu ametoa agizo hilo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa michezo wa Lwinga wilayani Namtumbo, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani Ruvuma.

“Nataka wananchi hawa wawe wamelipwa fidia yao ya ardhi kabla ya sikukuu ya Krismasi mwaka huu. Serikali haiko tayari kuona wananchi wake waliotoa ardhi kupisha maendeleo wakisumbuliwa.”

Jumla ya wananchi 21 wanaidai halmashauri ya Namtumbo eneo lenye ukubwa wa ekari 101,
ambazo mwaka 2008 zilitwaliwa na halmashauri ya wilaya hiyo kwa ajili ya kupisha ujenzi wa shule ya sekondari ya mkoa wa Ruvuma kwa ahadi ya kulipwa fidia jambo ambalo halijatekelezwa hadi leo.

Waziri Mkuu amesisitiza kuwa serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli inataka kila mtumishi ahakikishe anatumia taaluma yake vizuri kwa kuwahudumia wananchi ikiwa ni pamoja na kutatua kero zinazowakabili kwa wakati.