https://monetag.com/?ref_id=TTIb Usingizi Ni Muhimu Kwa Ustawi Wa Ubongo Wako | Muungwana BLOG

Usingizi Ni Muhimu Kwa Ustawi Wa Ubongo Wako

Mwili wa mwanadamu unauhitaji usingizi ili uishi maisha marefu, ujengeke, upate hamu ya kula, kunywa na kuvuta hewa. Ogani kubwa za mwili kama vile moyo, figo, ini na mapafu hufanya kazi yake vizuri wakati mtu amelala.

Kukosa usingizi kunaweza kusababisha kifo na mfano mzuri ni mwanamuziki, Michael Jackson ambaye alifariki baada ya kuzidishiwa dawa za usingizi.

Ni dhahiri kuwa baada ya shughuli nyingi za mchana kutwa, mwili wako unahitaji kupumzika kwa kulala usingizi.

Ila unachotakiwa kufanya si kulala usingizi ili mradi, bali usingizi safi ambao kitaalamu unatambulika kama, ‘hygienic sleep’.

Mwili wa mwanadamu unauhitaji usingizi ili uishi maisha marefu, ujengeke, upate hamu ya kula, kunywa na kuvuta hewa. Ogani kubwa za mwili kama vile moyo, figo, ini na mapafu hufanya kazi yake vizuri wakati mtu amelala.

Kutokana na sababu mbalimbali, wapo watu ambao wana tatizo la kutopata usingizi.

Tatizo hili kitaalamu huitwa, ‘Insomnia’. Ni ugonjwa ambao dalili zake ni pamoja na kushindwa kupata usingizi, kuamka mara kwa mara na kushindwa kulala tena kwa kipindi kirefu na kujisikia uchovu unapoamka.

Mtafiti wa usingizi, Dk Nathaniel Marshall kutoka Australia anasema kukosa usingizi kunaweza kukusababishia matatizo mbalimbali ikiwamo kujiweka katika hatari ya kifo.

Dk Marshall anasema uchunguzi alioufanya amegundua kuwa ajali nyingi mbaya za barabarani husababishwa na madereva wengi ambao hawajalala kwa zaidi ya saa 16.

Katika utafiti huo aliouchapisha mwaka jana, mtaalamu huyo alisema siyo tu kukosa usingizi kunaweza kusababisha ajali lakini pia kunaweza kumfanya mtu akose hekima.

“Mtu akikosa usingizi kwa muda mrefu siyo tu ana hatarisha maisha yake lakini pia anakosa busara, anaweza’ kuropoka’, au kufanya uamuzi mbaya ambao kama angelala vizuri asingeyafanya hivyo,” anasema Dk Marshall.

Daktari Bingwa wa Upasuaji nchini, Aidan Njau anasema kukosa usingizi (insomnia) kunaweza kusababisha kifo na mfano mzuri ni mwanamuziki, Michael Jackson ambaye alifariki baada ya kuzidishiwa dawa za usingizi.

Dk Njau anasema mtu anapokosa usingizi kwa muda mrefu anaweza kutumia njia yoyote kuutafuta na nyingi huwa za hatari ikiwamo kutumia dawa za usingizi au za kulevya.

“Ni rahisi mtu kujiingiza katika matumizi ya dawa za kulevya au za usingizi za kawaida, lakini hizi si nzuri kwani zikitumika kwa muda mrefu zinatengeneza ‘uteja,” anasema Dk Njau.

Aidha, anasema kuwa mwili wa binadamu unahitaji kulala ili kupumzisha ubongo ambao hufanya kazi nyingi pale mwili unapokuwa katika shughuli za mchana kutwa.

“Unapolala, ubongo unaingia kazini kutafakari matukio ya kutwa nzima na kutunza kumbukumbu. Kazi ya kuhifadhi kumbukumbu hufanyika unapokuwa umelala, “anasema na kuongeza.

“Ukikosa usingizi ni rahisi kuwa na tatizo la kusahau (memory loss) kwa kuwa ubongo haupati nafasi ya kufanya kazi yake ya kuhifadhi kumbukumbu hizo,” anasema.

Anaongeza kuwa usingizi husaidia kurekebisha seli zilizoharibiwa na msongo wa mawazo hasa zile ambazo hujitokeza dhahiri katika ngozi.

“Msongo wa mawazo, mionzi ya jua na kemikali husababisha seli za ngozi kuharibika. Mtu anapolala mwili huzalisha protini nyingi ambazo husaidia kuponya seli zilizoharibika,” anaeleza.

Anaongeza : “Ndiyo maana mtu asipolala ni rahisi kuona ngozi yake ikikunjamana na kukosa nuru nzuri kwa kuwa kile kitendo cha urekebishaji seli hakikupata nafasi”.

Daktari wa Bingwa wa magonjwa ya ndani ya mwili katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Raymond Mwenesano anasema sababu nyingi zinaweza kuwa chanzo cha kukosa usingizi ikiwemo ya kutumia vinywaji au dawa zenye kiambatanishi kiitwacho ‘caffeine’.