Sakata La Kanisa Katoliki Lahamia Bungeni


SAKATA la Kanisa Katoliki juu ya kuwapo madai ya ukabila limetinga bungeni, huku chombo hicho cha kutunga sheria kikiweka msimamo kuwa hakiwezi kutumika kama uwanja wa kuzungumzia masuala ya kidini.


Hata hivyo, bunge limesema linaweza kuzungumzia masuala ya dini iwapo yatawasilishwa kwa hoja mahsusi itakayowasilishwa kwa utaratibu unaokubalika katika kanuni zake.

Kauli hiyo ilitolewa bungeni jijini Dodoma jana na Mwenyekirti wa Bunge, Andrew Chenge, alipomjibu Mbunge wa Ndanda, Cesil Mwambe (Chadema).

Mara tu baada ya kumalizika kwa kipindi cha 'Mswali' bungeni jijini hapa jana asubuhi, mbunge huyo alisimama na kuitaka serikali itoe kauli kwa kile alichodai moja ya magazeti nchini lilichapisha jana habari zinazochonganisha waumini wa Kanisa Katoliki.

Alidai habari zilizochapishwa na gazeti hilo zinazodai kanisa hilo kuingia kwenye mgogoro, zinawachonganisha maaskofu na waumini kuamini uwapo wa ukabila ndani yake, hivyo kuitaka serikali kulitolea kauli suala hilo.

"Serikali ina 'regulate' (inasimamia) mambo mbalimbali yakiwamo ya kidini.  Pia mambo yote yanayowahusu wananchi. Lakini kumeibuka mambo na mivutano ambayo tumemwona Mheshimiwa Jenista (Mhagama - Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu) akiyakemea hasa zaidi yanayogusa imani za watu," Mwambe alisema.

"Kwa muda wa wiki moja mfululizo, gazeti limekuwa likiandika habari za kidini zinazojielekeza kwenye uchochezi kutaka kugombanisha watu na makabila yao. Kutaka kugombanisha watu wenye imani ya kikristo hasa kikatoliki.

"Huu ni uchochezi ambao unaweza kufarakanisha watu hasa ndani ya Kanisa Katoliki. Sasa tunaomba kauli ya serikali na mwongozo wako kuhusu uchochezi huu," alisema Mwambe.

Mwambe alisema anasikitika kuona Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe, hachukui hatua zozote dhidi ya gazeti hilo.

Katika majibu yake kwa mbunge huyo, Chenge alisema kuwa licha ya mwongozo huo kutokidhi matakwa ya kikanuni, kuna haja serikali kulifanyia kazi suala hilo.

Katika majibu yake kwa mbunge huyo, Chenge alisema kuwa licha ya mwongozo huo kutokidhi matakwa ya kikanuni, kuna haja serikali kulifanyia kazi suala hilo.
"Waheshimiwa wabunge, nimeombwa mwongozo kwa mujibu wa Kanuni ya 68(7). Kwa hilo alilolieleza halikutokea bungeni," Chenge alisema na kufafanua zaidi.

"Mwongozo wangu, kwa kuwa halikutokea humu bungeni, siwezi kusema kama linaruhusiwa kwenye kanuni zetu au la.

"Lakini serikali ipo humu na ina mikono mirefu na macho yanayoona mbali sana. Na sisi tumeweka msimamo kabisa isipokuwa kwenye hoja mahsusi itakayoletwa bungeni kwa utaratibu unaokubalika na Kanuni za Bunge.

"Bunge haliwezi kutumika kama uwanja wa kuongelea masuala ya dini. Kwa hiyo, naiachia serikali kama ikiona kuna haja ya kuyasemea, lakini naamini umesema kitu watakachokichukua kukifanyia kazi kwa taratibu."