Balozi Seif awataka mawaziri wa Afrika Mashariki kubadilishana uzoefu


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amewakumbusha  Mawaziri wa Wizara zinazofanana wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wale wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kukutana wakati unaporuhusu katika azma ya kubadilishana uzoefu kiutendaji ili kuboresha jukumu la kuwahudumia vyema Wananchi.

Alisema hatua hiyo muhimu ambayo ilikuwa ikifanyika katika kipindi tofauti itaendelea kujenga mapenzi zaidi, Umoja na Mshikamano  baina ya Watumishi wa Serikali zote mbili zilizopewa jukumu la kuwatumikia Watanzania wote.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa kumbusho hilo wakati akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ukiongozwa na Naibu Waziri wake Dr. Suzan Alphonce Kolimba ulipofika Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar kwa mazungumzo ya kubadilishana uzoefu.

Alisema Mikutano vikao vya mara kwa mara vya mazungumzo vitakavyowajumuisha  Mawaziri wa Wizara zinazofanana za pande hizo mbili hasa pale zinapojichomoza hitilafu ndogo ndogo katika pande mbili za Muungano husaidia kupunguza kero za Muungano.

“ Vikao vya mara kwa mara vya Mawaziri wa Wizara zinazofanana wale wa SMZ na SMT vina uwezo wa kupunguza au kuondoa kabisa vile vikao vya Watendaji Wakuu wanaokutana kujadili Kero zilizopo katika Muungano”. Alisema  Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliueleza Ujumbe huo wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwamba Wananchi wa Zanzibar na Tanzania Bara  Kihistoria ni wamoja kwa Karne kadhaa zilizopita kutokana na maingiliano yao ya Mila, Kibiashara, Silka na Utamaduni.

Balozi Seif alieleza kwamba udugu huo ndio uliopelekea Waasisi wa pande hizo mbili kufikia makubaliano yaliyowezesha kurasimishwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliozaa Tanzania mnamo Tarehe 26 Aprili Mwaka 1964.

Akitoa Shukrani kwa niaba ya Uongozi  wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Naibu Waziri wa Wizara hiyo  Dr. Suzan Alphonce Kolimba alisema kazi inayokabili Viongozi hasa Mawaziri Wapya ni kuendelea kupata mawazo na fikra za watangulizi wao ili jukumu walilokabidhiwa na Taifa walitekeleze kwa ufanisi uliotukuka.

Dr. Suzan alisema licha ya Taaluma waliyokuwa nayo Viongozi wachanga lakini bado busara na hekima za wale wazoefu zinapaswa kujumishwa pamoja katika utendaji wao kwa lengo la kuwatumikia vyema Wananchi walio wengi Mjini na Vijijini Tanzania Bara na Zanzibar kwa ujumla.

Viongozi hao wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wapo Zanzibar kwa shughuli za Kikazi likiwemo suala la kuratibu masuala ya Kimataifa  yanayojumuisha Serikali zote mbili ile ya SMT na SMZ.