Huu ndio mkwanja waliyovuta Ufaransa, Croatia

Michuano ya kombe la dunia kwa mwaka huu 2018 imemalizika nchini Urusi huku wapenzi wa soka wakishuhudia timu ya taifa ya Ufaransa ikitwaa taji hilo lililokuwa likishikiliwa na Ujerumani hii ni baada ya kuibuka na ushindi wa jumla ya mabao 4 – 2 dhidi ya Croatia.

Mchakato wa kumpata bingwa kwa mwaka huu ulihitimishwa hiyo jana kwenye dimba la Luzhniki baada ya kushuhudia jumla ya timu 32 zikimenyana katika kuhakikisha wanatwaa kombe hilo lililonakshiwa kwa dhahabu tupu.

Shirikisho la Mpira wa Miguu duniani FIFA liliongeza pato la bingwa wa michuano ya kombe la dunia kwa mwaka 2018 kutoka Dola 358 ya mwaka 2014 michuano ya Brazil hadi Dola 400 kwa mwaka huu ya huko nchini Urusi.

Kutokana na kuongezeka kwa kiasi hicho cha fedha kinamfanya mshindi wa kombe la dunia kwa mwaka huu 2018  ambaye ni timu ya taifa ya Ufaransa kuondoka na Shilingi bilioni 852 za Kitanzania pamoja na kikombe hicho cha dhahabu.

Kwa mujibu wa Shirikisho hilo kubwa kabisa duniani FIFA timu zote 16 zilizo tolewa kwenye hatua ya makundi ya michuano hiyo zimejiondokea na kitita cha dola milioni 8 kila moja wakati timu nane zilizopata bahati ya kutolewa hatua ya 16 bora zikijikusanyia dola milioni 12 kila moja.

Timu zilizotolewa hatua ya robo fainali ziliondoka na dola milioni 16 kila moja wakati timu ya taifa ya Uingereza iliyoshika nafasi ya nne ikifanikiwa kujinyakulia kitita cha fedha dola milioni 22.

Ubelgiji ambayo imefanikiwa kumfunga Uingereza na kushika nafasi ya tatu kwenye michuano hiyo ya mwaka huu iliondoka na dola milioni 24 huku timu ya taifa ya Croatia ambao wenyewe walishika nafasi ya pili ikiondoka na dola milioni 28 huku bingwa wa kombe la dunia mwaka huu 2018 Ufaransa ikijikusanyia dola milioni 38.

Kabla ya kuanza kwa kombe la dunia mwaka huu Shirikisho la Mpira wa Miguu duniani FIFA lilitoa kiasi cha dola milioni 1.5 kwa timu zote 32 ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea michuano hiyo wakati ikipeleka dola milioni 209 kwa klabu zote ambazo zimetoa wachezaji wake kushiriki kuchezea mataifa yao nchini Urusi na dola milioni 134 kama kinga kwa wachezaji ama bima endapo watapata majeraha. Fainali za mwaka huu 2018 FIFA iliongeza dola milioni 791 sawa na asilimia 40 ambazo ni zaidi ya michuano ya kombe la dunia iliyofanyika nchini Brazil mwaka 2014.