Vigezo Wanavyotumia Wanawake Kupenda Hushangaza


Watu wengi hujisikia vizuri wanapowavutia wenzao wa jinsia nyingine. Je, unafikiri ni kitu gani kinachomfanya mwanamke aonekane wa kuvutia?

Kuna vitu vingi vinavyojulikana vizuri zaidi kwa upande wa mwanamke kama vile; mwili mzuri, sauti yenye mvuto, nywele, mikono mizuri na mengineyo mengi. Lakini, kuna vingine ambavyo siyo vya kawaida vinavyohusu mwanaume kumvutia mwanamke.

Je, ni vitu au mambo gani ya kipekee ambayo, humfanya mwanamke aguswe na mwanaume fulani na huku mwanamke mwingine akishangaa ni kwa nini mwanamke mwenzake ameguswa sana na huyo jamaa?

Inawezekana yapo mengi ambayo, huyajui. Kwa mfano, mwanamke anaweza akavutiwa na jina la kwanza au la ukoo la mwananume fulani. Hapa mwanamke hufikiri kwamba, huyo mwenye hilo jina hawezi kuwa mtu wa kawaida, na kila kitu anachofanya ni lazima kiwe cha ajabu.

Labda ni kutokana na jina hilo kuwa ni la kigeni au anatoka kwenye ukoo ambao ni bora au wa kipekee au anafikiri labda huyo mwanaume atamwezesha kile ambacho, mara nyingi amekuwa hakipati.

Lakini, inawezekana kabisa kwamba, mwanamume huyo si mzuri sana wa kuvutia au ni mbaya sana kuliko wengine. Hakuna anayejua, labda anachotaka mwanamke huyo ni kujaribu bahati yake ili aone kitakachotokea kwa uhakika ziadi.

Inawezekana pia kuwa, mwanamke anaweza kuchanganyikiwa zaidi baada ya kuona umbo la mwanamume huyo au gari lake. Pengine mambo hayo ndiyo ambayo, amekuwa akiyapenda zaidi. Inawezekana ikawa ni dalili ya bahati kwake kwamba, ametokea katika maisha yake mtu ambae, kwa muda mrefu amekuwa akitamani kumpata.

Upo uwezekano pia kwamba, mwanamke akavutiwa na mwandiko au sahihi ya mwanamume fulani. Wakati mwingine mwanamke hutokea kuwa na uhakika zaidi na kuamini yale anayoambiwa kuhusu tabia ya mwanaume huyo, bila hata kufanya uchunguzi wa kina. Hata hivyo, ukweli ni kwamba, upo uwezekano wa kuisoma tabia ya mwanaume huyo kwenye sahihi au mwandiko wake.

Mwanamke pia huvutiwa na lafudhi ya mwanamume, fani yake, hobi, na kitu kingine kisicho cha kawaida ambacho mwanamume huyo anakipenda na kukifanya. Hata hivyo, mwanamke anatakiwa awe mwangalifu mno na upande wa pili wa mtu huyo ambao, yeye haujui. Hapa ikiwa na maana kuwa , pamoja na sifa zote hizo alizozibaini kutoka kwake, anapaswa kujua kwamba, mwanamume huyo kama binadamu asiyekamilika pia ana mapungufu na udhaifu mwingi.

Kuufahamu ukweli huu, kutamsaidia katika kuimarisha zaidi na kumfanya awe makini anapotafuta mwanaume wa kuishi naye. Na akumbuke kuwa, wapo wanaume ambao huficha makucha yao au kasoro zao kwa wapenzi wao.

Kuna mwanamke mwingine hupenda mwanaume mwenye vituko, kilema au mwenye kasoro nyingine za kimwili. Yote hayo hutokana na asili ya mwanamke. Na ni mambo yanayoongea ndani mwake kwamba, anataka kumjali na kumhurumia mwanaume huyo.

Kwa kawaida, mwanamke huvutiwa zaidi na kwa urahisi, pale mwanaume anapoonyesha tabia ya usikivu na utulivu. Hata hivyo, mtazamo huu kwa upande wa mwanamke, huhesabika kuwa ni ushindi kwake.

Hali kadhalika, mwanamke huvutiwa na tabia fulani ya kipekee ambayo, mwanaume anayo. Kwa mfano, jinsi mwanaume huo anavyoutumia mkono wake wa kushoto, kwani watu wengi wanatumia mkono wa kulia. Ukweli ni kwamba, labda huyo ndiye mwanaume ambae mwanamke huyo anamtaka, kwani pia wanawake wengine hawawezi kujizuia kuwapenda wanaume wenye macho ya bluu. Hilo pia ni jambo la kawaida.

Mwanamke anaweza kumpenda mwanaume kutokana na jinsi anavyofanya kazi za nguvu au kutokana na mwili wake kuwa na misuli. Ni jambo la kawaida kwa wanawake kufurahia wanaume waliojazia, na inavyoonekana wanawake huwaona wanaume ambao ni lainilaini kuwa wana haiba ya kike au ni mashoga.

Hapo ndipo mwanamke anapolazimika kufikiria kwa makini, kuhusu mwanaume anayetumia muda mwingi kujipodoa na fedha nyingi kwa mambo ya urembo na vipodozi kuliko hata mwanamke, kama kweli anamvutia na anamfaa.

Na kitu kingine ni kwamba, mwanamke humpenda mwanaume anayesaidia kufanya kazi za nyumbani. Kwa kufanya hivyo, mwanamke huamini kwamba, mwanaume huo anamjali na kumthamni.

Kwa kumalizia ni kwamba, mambo mengi yanayomchanganya mwanamke kuhusiana na mwanaume anayemtaka, kwa kweli ni ya kipekee sana na wakati mwingine huonekana kuwa ni kituko, ingawa wakati mwingine yanaweza yakaeleweka vizuri. Mara nyingi vigezo hivyo huonekana kuwa sahihi, iwapo tu mwanamke huyo atajisikia vizuri na kupata ridhiko la nafsi yake.