Ndalichako ataka Afisa manunuzi kusimamishwa kazi

Na Edina Fidelis

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. JOYCE NDALICHAKO amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo kumsimamisha kazi afisa manunuzi wa wizara hiyo kwa kununua vifaa vya maabara ambavyo havihitajiki katika chuo cha ualimu MOROGORO.

Prof. NDALICHAKO ametoa agizo hilo mara baada ya kutembelea maabara za fizikia, kemia na biolojia zilizopo katika chuo hicho na kubaini kuwepo kwa vifaa na kemikali ambavyo havitumika chuoni hapo.

Ziara ya siku moja ya  Waziri wa Elimu , Sayansi na Tekenolojia Prof. JOYCE NDALICHAKO mkoani MOROGORO, ambapo amefika katika shule ya sekondari ya MZUMBE na chuo cha ualimu MOROGORO.

Akiwa katika chuo hicho cha ualimu akatembelea maabara za fizikia, kemia na baiolojia ambako amekutana na masuala yaliyomkera na kutoa maagizo ya kuwasimamisha kazi baadhi ya wakufunzi na afisa manunuzi wa wizara hiyo.

Katika hatua nyingine Prof. NDALICHAKO amezungumza na wanafunzi na walimu wa shule ya sekondari MZUMBE na kuipongeza kwa kufanya vizuri katika mitihani ya kitaifa na kupokea taarifa ya ukarabati wa miundombinu ya shule iliyosomwa na mkuu wa shule WENCESLAUS KIHONGOSI.