Bondia Hassan Mwakinyo aweka wazi maandalizi yalivyomtesa mpaka kufika Uingereza


Jina la Hassan Mwakinyo kwa sasa siyo geni tena masikioni mwa Watanzania wengi - Tena baada ya kumtwanga bondia wa Uingereza, Sam Eggington katika raundi ya pili kwa Knock Out.

Bondia huyo Ijumaa hii ametembelea katika Bunge la Jamuhuri ya Tanzania kusalimiana na wabunge pia ameelezea ugumu alioupata katika maandalizi yake ya mchezo huo uliomtangaza vema. 

Akiongea na waandishi wa habari nje ya ukumbi huo wa wa Bunge, Hassan amesema, "Nimeondoka Tanzania kama mfungwa, kama mkimbizi, hata pesa ya kulipia visa ilikuwa shida kuipata, nakumbuka hata nauli tu ilibidi nikope pesa ya ada ya mwanafunzi,"

"Nimepigana Uingereza bila sapoti yoyote, lakini namshukuru Mungu nimeshinda, wapo wengi wanasema ni mameneja wangu, niseme tu kwamba ni waongo, hakuna mtu anayenimeneji, wala aliyetoa pesa yake mfukoni kunigharamaia,” ameongeza.