Hatma ya makontena ya Makonda hii


Baada ya minada mitatu iliyofanyika kushindwa kupata mnunuzi wa makontena 20 ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) sasa inafanya taratibu za kuyatoa bandarini ili kuyagawa bure katika taasisi za kiserikali na pamoja hospitali.

Akizungumza na www.eatv.tv Kamishana Mkuu wa TRA, Charles Kichere amesema kuwa yatagawiwa bure hivi karibuni kwani sheria inaruhusu kugawa katika taasisi za kiserikali na sio binafsi pamoja na maeneo yoyote yenye huduma za kijamii, endapo mali inapokosa mteja.

“Sheria inaturuhusu kugawa popote kwenye huduma za kijamii ikiwemo hospitali, kwakuwa minada yote hakuna mnunuzi aliyepatikana, kuna utaratibu ulioelekezwa kisheria wa kuziondoa mali hizo sehemu ya mnada na moja ya utaratibu huo ni kugawa bure”, amesema Kamishna Kichere.

Mara ya kwanza makontena hayo yalipigwa mnada Agosti 25, lakini yalikosa wanunuzi, watu wengi walishindwa kufikia bei iliyotakiwa, baadhi wakitaja Shilingi milioni 10 kwa kontena badala ya Shilingi milioni 60 inayotakiwa, baaada ya makontena hayo kutouzika ambapo Agosti 26, Makonda alitoa onyo akiwa mkoani Kagera kuwa atakayeyanunua atalaaniwa yeye na uzao wake.

Agosti 27, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Phillip Mpango alikwenda bandarini kuyakagua na kuwataka viongozi wenzake serikalini kutathmini kauli zao na akawaomba wanaotaka kuyanunua wasiogope.

Akizungumza na madiwani, viongozi na watumishi wa Halmshauri ya Wilaya ya Chato mkoani Geita, Agosti 30, Rais John Magufuli alizungumzia sakata hilo akiwataka viongozi kuwatumikia wananchi bila kujali wapo kwenye nafasi gani.

“Umesikia hili sakata la Dar es salaam, eti Mkuu wa Mkoa ameleta makontena, ameambiwa alipe kodi, kwa nini asilipe kodi?” Alihoji Rais Magufuli. Sheria za nchi zinasema ni mtu mmoja katika nchi mwenye dhamana ya kutolipa kodi kwa mujibu wa sheria ya fedha, sheria ya madeni, sheria ya dhamana na ya misaada.

“Sasa ukichukua makontena kule umezungumza na watu wengine labda na wafanyabiashara, unasema ni makontena yako halafu ukasema tena labda ni ya walimu, wala hata shule hazitajwi maana yake nini”.