Kuna faida kubwa wa faragha na makosa ya mwanamke


TENDO la ndoa lina umuhimu wake. Kwa namna moja au nyingine linakamilisha maana nzima ya mapenzi. Ni kama vile kachumbari kwenye pilau. Si kwamba pilau haliliki bila kachumbari lakini ikiwepo, utamu unakamilika. Ili kuleta ustawi wa penzi, mwanamke ana wajibu wa kutenda tendo hilo kikamilifu, hali kadhalika mwanaume. Mmoja kati yao anapolifanya chini ya kiwango, humuweka mwenzake njia panda. Aone kuna kitu hakijakamilika.

Hakijakamilika kwa sababu amemuacha njiani. Mwenzake alikuwa anahitaji kuendelea na safari, lakini yeye ameikatisha. Ni sawa na mtu kuwa na kiu ya maji halafu, ukapewa maji kiduchu. Kiu inabaki palepale, unatamani kupata maji mengi ili uikomeshe lakini mwenzako hana habari.

Kwa kuwa uhusiano unajengwa na vitu vingi likiwemo hilo, linapokuwa linafanyika chini ya kiwango, uhusiano unakuwa haujakamilika. Upungufu utaonekana na taratibu penzi linaweza kuyumba. Kachumbari ikikosekana kwenye pilau, ladha itatoka wapi?

Nirudi kwenye msingi wa hoja sasa. Kwa kuzingatia kwamba unyumba ni kiunganishi adimu kwenye uhusiano, baadhi ya wapendanao hususan wanawake hupenda kutumia nafasi hiyo kuwanyanyasa wenzi wao. Wanaugeuza unyumba kuwa fimbo ya kuwachapia wenzi wao.

Mwanamke anaona ili kumkomoa mwanaume kutokana na kosa fulani, anamnyima unyumba. Anaamini ni silaha kubwa. Kwamba mwanaume aliyekamilika, lijali kabisa, hata iweje lazima atakuwa na hitaji hilo la mwili. Atahangaika huku na kule akiwa faragha ili mradi tu akate kiu yake. Nimesema wanawake wengi hupenda kuitumia silaha hiyo maana kwa sababu kimaumbile, wao ni rahisi sana kujizuia kuliko wanaume.

Wanaamini wanaume si wavumilivu. Watahangaika, mwisho wa siku watahitaji tu ‘huruma’ ya wanawake. Penzi wanaligeuza kama hisani. Yeye ndiye mmiliki wa tendo hilo. Anataka atafanya, asipotaka basi hakuna kitakachoeleweka. Wanaamini kwamba ili mwanaume apewe, inabidi awe mpole. Ajishushe. Kama alikosea, anapaswa kuomba kwanza msamaha, asamehewe ndipo mambo yaendelee. Vinginevyo ataishia kulala mzungu wa nne.

Itakuwa siku, wiki, mwezi na hata miezi kadhaa. Hadi kieleweke. Mwanaume akubali kujishusha, apewe unyumba. Asipofanya hivyo kazi anayo. Aandike maumivu endelevu mpaka pale atakapoamua kujishusha na kutambua thamani ya mwenzi wake.

NI KOSA KUBWA
Si busara kutumia unyumba kama silaha ya kumchapia mwenzako pale anapokosea. Ni bora ukamuadhibu kwa mambo mengine lakini si unyumba. Kile ni kiunganishi muhimu, kinapokosekana, madhara yake ni makubwa. Usaliti huanzia hapo. Kumnyima mwenzi wako unyumba, ni kukaribisha mwanya wa usaliti. Atavumilia, naye ni binadamu anaweza kuchoka. Anaweza kutafuta jinsi ya kufanya. Akiifanya, akinogewa unafikiri nini kitatokea? Hataona umuhimu wako.

Atakulinganisha wewe na yule aliyechepuka naye. Ataona amepata tiba sahihi. Ni rahisi kukufanya wewe ni mlezi wa familia. Mwanamke naye akigundua, naye anaweza kuona njia nzuri ya kumkabili ni kujibu mapigo. Hapo ndio kunakuwa hakuna mapenzi. Kama ni ndoa itakuwa rehani. Muda wowote inaweza kuvunjika, kila mmoja akachukua njia yake.

UNYUMBA SI PROMOSHENI
Chondechonde, usimpe mwenzi wako unyumba kama vile unamzawadia. Mpe kama ni wajibu wako. Ona kabisa una kila sababu ya kumpa maana wewe ndiye kimbilio lake. Wewe ndiye unayepaswa kumtimizia mahitaji yake ya kimwili, kiakili na hata kifikra.

Kama amekosea, kasirika, nuna, baadaye hasira zikiisha, mueleze pale alipokukwaza. Kama binadamu, atajipima na ataelewa makosa aliyoyafanya. Hata kama mna ugomvi, linapokuja suala la unyumba hupaswi kulifanyia mzaha maana ni hatari kwa mustakabali wa penzi lenu.

TENDO NI MUHIMU KWELIKWELI
Kwanza ndivyo tafsiri rahisi ya vitabu vya dini. Vinasema, enendeni mkaijaze dunia. Hamuwezi kuijaza dunia pasipo kufanya tendo hilo. Utofauti wake tu, kuna wanaolifanya kihalali kwa maana ya kufunga ndoa kwanza lakini kuna wengine wanaanza kushiriki kabla hata hawajafunga ndoa!