Mwanafunzi Atiwa Mbaroni Kwa Kutupa Mtoto Chooni

JESHIi la Polisi Mkoa wa Mbeya linamshikilia mwanamke mmoja ambaye amefahamika kwa jina la INES MTUNDU [19] Mwanafunzi wa Kidato cha Nne katika Shule ya Sekondari Isengo kwa kosa la kumtupa chooni mtoto mchanga wa masaa kadhaa.

Tukio hilo limetokea mnamo tarehe 23.09.2018 majira ya saa 09:53 asubuhi huko maeneo ya Isengo – Airport ya zamani, Kata ya Iyela, Tarafa ya Iyunga, Jijini Mbeya. Inadaiwa kuwa mwanafunzi huyo alikuwa mjamzito na mara baada ya kujifungua chooni ndipo alimtupa mtoto huyo.

Mara baada ya taarifa kulifikia Jeshi la Polisi, jitihada za haraka zilifanyika kwa kushirikiana na Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji na kufanikiwa kumuokoa mtoto huyo akiwa hai. Mama na mtoto huyo wote wapo Hospitali ya Wazazi – Meta wakipatiwa matibabu. Upelelezi unaendelea na mara baada ya kukamilika mtuhumiwa atafikishwa Mahakamani.