Updates: Idadi ya waliofariki kwenye ajali MV Nyerere yaongezeka


Mpaka sasa miili ya watu iliyoopolewa katika ajali ya kivuko cha Mv Nyerere imefikia watu 225 baada ya saba kupatikana usiku wa kuamkia leo Septemba 23, 2018.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkuu wa mkoa wa Mwanza, John Mongella amesema kuwa leo asubuhi miili saba imeopolewa na kufikisha idadi ya miili 225.

Kwa upande mwingine, Mhe. Mongella anasema baadhi ya maiti zilizokuwa zimezama chini ya maji, zimeanza kuibuka na kuelea na tangu alfajiri miili minne imeonekana na kuopolewa katika fukwe za Bwisya.

Tayari uchimbaji wa makuburi unaendelea kwa ajili ya maziko ya miili ambayo haijatambuliwa na amedai kuwa wapo marehemu waliotambuliwa na ndugu zao lakini wakaomba wazikwe katika utaratibu ulioandaliwa na Serikali.