https://monetag.com/?ref_id=TTIb Cheche za Katibu Mkuu CCM zamgusa Lowassa | Muungwana BLOG

Cheche za Katibu Mkuu CCM zamgusa Lowassa

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Edward Lowassa amempongeza Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt Bashiru Ally kwa kauli aliyoitoa hivi karibuni ya kuwa serikali ya 2010 haikuwa na uhalali kisiasa.

Lowassa ametoa kauli hiyo wakati akichangia kwenye mjadala wa Miaka 19 ya kumbukizi ya kifo cha hayati Mwalimu Julius Nyerere iliyofanyika Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM) ambapo wasomi mbalimbali walishiriki kwenye mjadala huo.

"Nimpongeze Katibu Mkuu mpya wa CCM, nimezisikia cheche zako, nasubiri Uchaguzi wa 2020 kama utarudia kauli yako kuhusu uchaguzi wa 2010. Pia nawaomba Chuo Kikuu msikae kimya kama ilivyokuwa wakati  wetu kwa matatizo yanayotokea nchini", amesema Lowassa aliyewahi kuwa Waziri Mkuu nchini.

 "Mi nadhani nchini kuna hofu kubwa sana ya uchaguzi, inafaa tutazame wasimamiaji wa uchaguzi kwa sababu wengi wanateuliwa na serikali na wengine wanasema wazi wamepewa kazi na serikali na ndio maana hakuna uchaguzi mdogo hata mmoja ambao Upinzani tumeshinda", ameongeza Lowassa.

"Ingefaa kuzungumza na wananchi wetu tuache chuki na hofu, tungekuwa na baraza la wazee la kuwaambia viongozi hili jambo si sawa na si kusema kuna viasharia vya uvunjifu wa amani.

Oktoba 14, 1999 ndio siku ambayo Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alifariki dunia wasomi mbalimbali wiki hii wamekutana ili kujadili fikra zake kulingana na mazingira ya sasa.