Mbunge Chadema amkosoa mwenzake aliyehamia CCM


Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi Kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Gibson Meiseyeki amekosoa madai ya aliyekuwa Mbunge wa Babati Mjini Pauline Gekul kuwa miongoni mwa sababu zilizopelekea kiongozi huyo kujiuzulu ni kuwepo kwa michango mingi ndani ya chama hicho.

Moja ya sababu ambayo Pauline Gekul aliitaja wakati akijiuzulu nafasi yake ndani ya CHADEMA hivi karibuni ni kutozwa michango mingi kwa wabunge licha ya chama hicho kupokea ruzuku ya milioni 300 kwa mwezi.

“ Kwa mwanachama wa chama chochote kuchangia ni lazima, ni kitu tunakipenda, mbunge kuchanga milioni 2 ni hela ngapi lakini kiukweli hakuna mbunge anayechanga milioni 2, ila kuna gharama kidogo ambazo hata wanaotumia kwenye mitandao wanazitoa.”

"Hata hivyo michango hiyo iko kimahesabu hakuna mtu anayeonewa, na hata hivyo haiwezi kuwa ajenda ya mtu kuhama chama bali ni umasikini wa fikra," Amesema Mbunge huyo.

Mapema mwezi huu, Mbunge mteule wa Jimbo la Ukonga Mwita Waitara aliwahi kunukuliwa akisema, "katika zile Arumeru mbili mbunge mmoja atahama muda si mrefu, na hapa Dar es salaam kuna mbunge mmoja atahama, nilisema wabunge watano wamesharudi wawili, tayari Marwa Ryoba, na James Ole Milya wamesharudi, kwa hiyo tutegemee jambo lolote kuanzia sasa kwa wabunge mkoa wa Dar es salaam na Arusha."