Simba SC yatangaza kusitisha mazoezi yake baada ya MO kutekwa


Kufuatia kutekwa na watu wasiojulikana kwa Bilionea na Mwekezaji wa Klabu ya Simba SC, Mohammed Dewji 'MO' uongozi wa Klabu hiyo umetangaza kuhairisha mazoezi ya timu hiyo.

Msemaji wa Simba, Haji Manara amesema hatua hiyo imefikiwa baada ya mashauriano baina ya uongozi na benchi la ufundi ili kutoa fursa kwa wachezaji na benchi hilo kushiriki dua maalum ya kumuombea MO.

" Baada ya makubaliano kati ya viongozi na benchi la ufundi tumeamua kusitisha mazoezi ili kushiriki kwenye dua hiyo maalum, tunawaomba tena na tena watanzania na wanaoitakia mema nchi yetu wasiache kumuombea uhai na uzima Bwana Mohammed Dewji," ameandika Manara.

Dewji ametekwa leo asubuhi wakatia akiingia kufanya mazoezi kwenye Hotel ya Colosseum ambapo taarifa hizo zilithibitishwa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa.