https://monetag.com/?ref_id=TTIb Kufuatia nyumba 27 kuezuliwa paa, wanaoishi maeneo hatarishi watakiwa kuhama | Muungwana BLOG

Kufuatia nyumba 27 kuezuliwa paa, wanaoishi maeneo hatarishi watakiwa kuhama



Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Joachim Wangabo amewaagiza wakurugenzi wote wa halmashauri kuhakikisha wanatekeleza sheria ya upandaji miti kwa kila nyumba ili iwe ngao dhidi ya upepo mkali unaosababisha maafa na kuwafanya wanachi hao kukosa mahala salama pa kukaa na wengine kuharibikiwa na vyombo vyao.

Ameyasema hayo alipokwenda kuwatembelea walioathiriwa na upepo mkali ulioambatana na mvua kubwa iliyoezua paa za nyumba zipatazo 27 na kusababisha hasara ya zaidi ya shilingi milioni 26 katika Tarafa ya kirando, Wilayani Nkasi.

“Mh. DC tuwe wakali katika hili, kuhakikisha kwamba nyumba ambayo haina miti inayozunguka lile eneo la makazi tuhakikishe kwamba tunachukua hatua stahiki za mazingira, halmashauri mnajua hata kwenye vibali vya ujenzi huwa mnasema lazima muwe na miti angalau minne kama sio mitano lakini hakuna anaefuatilia kwamba hiyo miti ipo? Sasa ni wakati muafaka wa kufuatilia taratibu zote,” alisisitiza.

Wangabo aliongeza kuwa wale wote waliojenga kwenye mabonde ya mpunga wajue kwamba maeneo hayo si salama na kama watapatwa na maafa yoyote wasiitegemee serikali kuwahudumia kwasababu serikali imeshatoa onyo juu ya uhatari wa makazi hayo na kuwataka wananchi wasiishi kwenye maeneo hatarishi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Nkasi, Said Mtanda amesema kuwa halmashauri ya Wilaya ya Nkasi inaendelea kutoa elimu ya ujenzi wa nyumba bora na katika kuhakikisha jambo hilo linatekelezwa kamati za ujenzi za vijiji zinaendelea kuundwa katika kila kijiji ikimabatana na jukumu la kuhamasisha upandaji wa miti.