Klabu ya Simba yatangaza kufanya usajili mwengine


Klabu ya Simba kupitia kocha wake mkuu, Patrick Aussems imesema kuwa ina mpango wa kuongeza mchezaji mmoja wa kimataifa kabla ya dirisha dogo la usajili kufungwa wiki hii.

Kocha Aussems ametaja mpango huo alipokuwa akizungumzia juu ya maandalizi ya mchezo pamoja na suala la usajili, katika programu ya mazoezi ya timu Jijini Dar es salaam, ambapo amesema, "nimewatazama Nkana, wako vizuri lakini kama ninavyoeleza kila siku kuwa kikubwa kwetu ni kuelekeza nguvu zetu kwenye kufanyia kazi mifumo ya kiuchezaji".

"Tunahitaji mchezaji mwingine mpya na tunatakiwa tumsajili kabla ya Jumamosi, Disemba 15 , kwahiyo nafikiri nitasajili mchezaji mmoja kabla ya siku hiyo. Anaweza kuwa ni kiungo, mshambuliaji au vinginevyo kwahiyo kutakuwa na taarifa ndani ya masaa 48 yajayo," ameongeza Aussems.

Simba ipo katika maandalizi ya mwisho ya mchezo wa hatua ya pili ya makundi ya Klabu Bingwa Afrika dhidi ya Nkana FC ya Zambia, mchezo utakaopigwa wikeendi hii nchini Zambia.

Kikosi hicho knatarajia kuondoka nchini Alhamisi ya wiki hii kuelekea nchini Zambia ambapo kitaondoka na mashabiki wake baada ya kutangaza utaratibu maalum kwa wanaotaka kwenda kuishangilia timu yao nchini humo.

Baada ya mchezo huo, itarejea nyumbani kwaajili ya mchezo wa marudiano na endapo itafanikiwa kuvuka hatua hiyo, itaingia katika hatua ya makundi ya michuano hiyo mikubwa barani Afrika.