https://monetag.com/?ref_id=TTIb Watu Sita wafariki dunia kwenye ajali Morogoro | Muungwana BLOG

Watu Sita wafariki dunia kwenye ajali Morogoro


Watu sita wamefariki dunia kwa ajali ya gari mkoani Morogoro, ambapo miongoni mwa waliofariki ni msanii maarufu wa muziki wa mchiriku na singeli kutoka kundi la 'Jagwa', Jack Simela.

Ajali hiyo imetokea katika eneo la Msamvu mkoani Morogoro, baada ya gari lao dogo lililokuwa likitokea kwenye mazishi mkoani humo kugongana uso kwa uso na lori aina ya Scania.


Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Morogoro, Dkt. Simon Tarimo, amethibitisha kupokea miili sita na majeruhi wawili, na kusema kwamba hali za majeruhi zinaendelea vizuri hospitalini hapo.

Chanzo cha ajali hiyo bado hakijawekwa wazi, baada ya jitihada za kumtafuta Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro kugong mwamba.

Jack Simela alikuwa ni muimbaji kiongozi wa kundi la Jagwa Music ambalo ni maarufu kwa muziki aina ya mchiriku, muziki ambao umekuwa ukipendwa na mataifa ya nje ikiwemo Ujerumani, ambako ndiko mara nyingi yeye na kundi lake walikuwa wakienda kufanya matamasha.