https://monetag.com/?ref_id=TTIb Tanzania ni miongoni mwa nchi iliyopiga hatua mapambano dhidi ya rushwa | Muungwana BLOG

Tanzania ni miongoni mwa nchi iliyopiga hatua mapambano dhidi ya rushwa


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema nchi za Bara la Afrika zimeitaja Tanzania kuwa ni miongoni mwa nchi zinazofanya vizuri katika mapambano dhidi ya rushwa.

Ameyasema hayo, wakati akitoa muhtasari wa yaliyojiri kwenye Mkutano wa 32 wa Wakuu wa nchi za Afrika (AU) unaofanyika Addis Ababa, Ethiopa.

Waziri Mkuu ambaye amemuwakilisha Rais Dkt. John Magufuli katika mkutano huo amesema katika mkutano huo pamoja na mambo mengine Serikali barani Afrika zimesisitizwa kupambana na wala rushwa, ambapo Tanzania imetajwa kuwa miongoni mwa nchi zilizopiga hatua katika mapambano hayo.

Mbali na kupiga hatua katika mapambano dhidi ya rushwa, pia Waziri Mkuu amesema ripoti ya kamati maalumu iliyoundwa kuhusu masuala ya afya inaonesha Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizofanya vizuri.

Waziri Mkuu amesema Tanzania imefanya vizuri katika kusimamia na kudhibiti malaria, mapambano dhidi ya ukimwi pamoja na utoaji wa huduma za afya kwa wananchi mpaka vijijini.

"Imetupa faraja kwa sababu ukaguzi uliofanywa na kamati maalumu ya maendeleo ya afya, iliyotembelea nchi za Afrika kuona mwenendo wa utoaji wa huduma za afya imeonesha kwamba Tanzania tupo kwenye kiwango kizuri.”

Waziri Mkuu amesema mafanikio hayo yamekuja baada ya Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli kuongeza bajeti ya afya wizara kutoka sh. bilioni 37 hadi kufikia sh. bilioni 269.

Kadhalika, Waziri Mkuu amesema viongozi hao walizungumzia kuhusu mwenendo wa biashara kwa kutumia anga, bahari na biashara za nchi kavu ambazo zinafanywa na Bara la Afrika na Tanzania ni miongoni mwa ambazo zilikubaliana na uundwaji wa mkataba wa korido ya biashara.

Amesema viongozi hao wametakiwa waimarishe biashara na Serikali imetoa fursa ya wazi kwa wafanyabiashara wa ndani na nje waje wawekeze na Tanzania iko tayari kuungana na Mataifa yakayofanya biashara nchini.

Katika mkutano huo, viongozi wa AU wamekutana kwa ajili ya kujadili masuala mbalimbali kuhusu biashara, wakimbizi na usalama, pia wamemchagua  Rais wa Misri, Abdul Fatta Al Sisi kuwa Mwenyekiti mpya wa umoja huo.

Al Sisi anachukua nafasi hiyo kutoka kwa Rais wa Rwanda Paul Kagame kumaliza muda wake baada ya kushika wadhifa huo kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Antonio Guterres amesema licha ya changamoto zote zinazolikabili bara la Afrika, bara hilo limeacha milango yake wazi kwa wakimbizi, hivyo ameyataka nchi za Ulaya ambazo zimefunga milango yake kwa wakimbizi zijifunze kutoka kwa Afrika.

Guterres ameyasema hayo katika Mkutano Mkuu wa 32 wa viongozi wa nchi wanachama za AU ambao kauli mbiu  ya mkutano wa mwaka huu nı ” Wakimbizi na waliorejea makwao”.

Kiongozi huo wa AU ameongeza kuwa Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa unakabiliwa na changamoto kuu tatu ambazo ni amani na usalama, maendeleo endelevu pamoja na mabadiliko ya hali ya hewa.