Wanafunzi wafunguka wanavyorubuniwa, kupewa ujauzito


Wanafunzi wa kike wameelezea namna wanaume wanavyowarubuni na kusababisha baadhi yao kupata ujauzito na kulazimika kukatisha masomo.

Wanafunzi hao waliyasema hayo wakati wa kampeni ya kupambana na tatizo la ndoa na mimba za utotoni inayoendeshwa na Shirika linalojishughulisha na masuala ya kisaikolojia kwa watoto (REPSSI) katika vijiji na mitaa iliyo pembezoni kwa barabara ya Kilwa, Dar es Salaam.

Simulizi za wanafunzi hao katika maeneo tofauti ziliwafanya wapigwe butwaa kutokana na kutotaja sababu za mimba.

Lakini mwanafunzi wa darasa la sita katika Shule ya Msingi Bungu B, Kibiti mkoani Pwani aliweka bayana mbinu hizo baada ya kuulizwa sababu za tatizo la mimba na ndoa za utotoni.

“Wengi hujikuta wakiangukia kwenye mitego kutokana na ahadi kemkem,” alisema huku akishangiliwa.

“Ngoja mie niseme ukweli. Utakuta baba anakukaribisha chipsi wakati huo umetoka shule una njaa na nyumbani ni mbali. Ukila tu anaanza kukuahidi kuwa ukiwa mkubwa atakujengea nyumba na kama utakubali anachotaka mara atakuwa anakupa hela za nauli shuleni.

“Mimi ni mtoto ila kuna mtu mkubwa aliwahi kuniambia ujinga nikamsemea kwa mama akasema nisikubali tena kusikiliza hao watu waongo, wabaya. Wakiniharibu watakimbia.”

Alisema wasichana wanatakiwa kutimiziwa mahitaji yote muhimu ili isiwe rahisi kurubuniwa,
Ukipata mimba unafukuzwa shuleni na nyumbani wazazi hawakuelewi lakini njiani vishawishi vinazidi uwezo wa mtoto kuhimili.