Waziri awaonya wanaowamendea wanafunzi kimapenzi


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu amewataka wazazi na walezi kuacha tabia ya kuwakandamiza watoto wa kike na kuwanyima haki zao za msingi ikiwa ni pamoja na kupata elimu.


Waziri Ummy amesema hayo katika ufunguzi wa mkutano wa mradi wa Elimu kwa Wasichana inayotekelezwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia uliofanyika unaoendelea katika Hotel ya Hyatt Jijini Dar Es Salaam. “Serikali ya awamu ya tano imechukua hatua mbalimbali kuhakikisha Wasichana wanapata elimu bila vikwazo vya kuolewa mapema ama mimba za utotoni, kubwa ni uamuzi wa Rais John Pombe Magufuli kufuta ada kwa wanafunzi wa msingi na sekondari lengo ni kuhakikisha kila mtoto wa kike anapata haki sawa ya elimu kama mtoto wa kiume”. Amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy amesema ili kupambana na mimba za utotoni Serikali imefanya mabadiliko ya Sheria ya Elimu ambapo hivi sasa mtu yeyote akioa au kuolewa na mwanafunzi wa Shule ya msingi anakua ametenda kosa la jinai na adhabu yake ni kifungo kisichopungua miaka 30 jela.

Aidha, Waziri Ummy amesema Serikali imeboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia ambapo katika kipindi cha mwaka 2018 mabweni zaidi ya 530 yamejengwa katika shule mbalimbali za sekondari na kwa kiasi kikubwa wanakaa watoto wa kike ili kujiepusha na vishawishi na hatimaye kupata mimba za utotoni.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha amesema ndoa za utotoni zinamfanya mtoto wa kike kupoteza uelekeo wa maisha yake hivyo Serikali katika kupambana na hilo inahakikisha watoto wa kike wanabaki mashuleni na kuwekewa mazingira wezeshi lakini pia kutoa ushauri ili waweze kujua afya zao na kuepuka mimba za utotoni.