Zahera: Tatizo lililotokea katika mchezo ni wachezaji wetu kukosa ubunifu


Kocha Mkuu wa Yanga SC, Mwinyi Zahera amefunguka kuwa licha ya timu yake kufungwa na watani wao Simba, itawapiga msimu ujao wakiwa wamejipanga kwakuwa Simba inacheza mpira wa kawaida.

Zahera amesema hayo jana mara baada ya timu yake kufungwa bao 1-0 na kusema kuwa Simba inacheza mpira wa kawaida sana na wao wakijipanga msimu ujao watawashangaza wapinzani wao.

"Tatizo lililotokea katika mchezo wa leo ni wachezaji wetu kukosa ubunifu, leo (jana) namna Simba inacheza ni rahisi sana kuwapiga lakini mwaka ujao timu nitakuwa nayo kwasababu wachezaji nilionao sasa hivi sio mimi niliyewachagua", amesema Zahera.

Hata hivyo kocha huyo amewapongeza Simba kwa mchezo huo na akikiri kuwa kiwango cha mchezaji mmoja mmoja cha wachezaji wake na wa Simba ni tofauti.

Simba imeshawasili mkoani Arusha tayari kwa maandalizi ya mchezo ujao wa ligi dhidi ya African Lyon utakaopigwa Februari 19 katika uwanja  wa Sheikh Amri Abeid, huku Yanga ikitarajia kusafiri hadi Jijini Mwanza kuvaana na Mbao FC.