LAAC yatoa maagizo matano kwa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba


Na Sylvester Raphael

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) yatoa maagizo matano kwa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba baada ya kubaini ubadhilifu wa zaidi ya shilingi bilioni 1.4 kutumika kinyume na taratibu kanuni na sheria za fedha kutokana na uzembe wa baadhi ya wataalamu katika Halmashauri hiyo ya Manispaa ya Bukoba.

Pia ni baada ya  Kamati hiyo ya Bunge kugundua kuwa asilimia 90% ya miradi iliyotekelezwa mwaka wa fedha 2015/16, 2016/17 na 2017/18 ilitekelezwa chini ya kiwango ikiwa ni pamoja na udhaifu mkubwa wa kamati ya fedha ya Halmashauri hiyo  katika usimamizi wa miradi ya maendeleo na kutokana na sababu hizo mbili Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Vedasto Edga Ngombale Mwilu ilitoa maagizo yafuatayo;

Agizo la Kwanza: ni kuhusu mradi wa ujenzi wa madarasa na ukarabati wa miundombinu ya shule ya Sekondari Rwazi, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera iliagizwa kufuatilia mradi huo na kuhakikisha ujenzi na ukarabati unakamilika kabla ya Mei 30, 2019 na taarifa ya utekelezaji wa mradi huo ifike ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali pamoja na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) tarehe 1 Juni, 2019.


Agizo la pili: Kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo, Kamati ya Bunge ya Serikali za Mitaa (LAAC) iliagiza Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kufanya ukaguzi maalum wa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba na ukaguzi huo utahusisha mwaka wa fedha 2015/16, 2016/17 na 2017/18 na taarifa hiyo ya ukaguzi maalum ikikamilika iwasilishwe mapema iwezekanavyo mbele ya kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa.

Agizo la tatu: Wakati Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) akiendelea na ukaguzi Afisa Masuhuli na Mkurungenzi wa Manispaa ya Bukoba anatakiwa kuchukua hatua za kisheria na kinidhamu kwa watendaji wote waliohusika na ubadhilifu wa fedha za Serikali katika Miradi hiyo.

Agizo la nne: Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ikishirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba washirikiane kubaini Mkandarasi aliyepewa tenda ya kutekeleza miradi minne lakini hadi sasa hajulikani na hajitokezi kudai madai ya fedha zake za utekelezaji wa miradi hiyo aidha, ofisi hizi mbili zimpate Mkandarasi huyo kupitia vyombo husika BRERA au Vyombo vya Ulinzi na Usalama.

Agizo la tano:  Kuhusu nafasi za Wakuu wa Idara wanaokaimu, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ikishirikiana na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) pamoja na Ofisi ya Menejiment ya Utumishi wa umma wahakikishe nafasi zote zinazokaimiwa wanaokaimu kama wanazo sifa wapewe ukuu wa idara na kama hawana sifa waletwe wakuu wa idara katika nafasi hizo ili kuimarisha utendaji katika Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba.


Kamati hiyo ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa ilitoa maagizo hayo matano Machi 22, 2019 kwa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba baada ya kutembelea na kukagua miradi mitatu walioitilia mashaka utekelezaji wake lakini pia Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) alikuwa imeitilia mashaka na kubainisha mapungufu makubwa katika taarifa yake, aidha, miradi iliyotembelewa ni kama ifutavyo.

Mradi wa barabara kilometa tano wa rami ngumu uliofadhiliwa na Benki ya Dunia wenye thamani ya shilingi bilioni 7, katika Mradi huo alipewa tenda Mkandarasi NCL wa Jijini Dar es Salaam na ulitakiwa kuanza Juni 19, 2018 na kukamilika Aprili 18, 2019 lakini baada ya Mkandarasi kuanza kazi aliutelekeza mradi huo kabla haujakamilika na  Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba ilikuwa tayari imemlipa kiasi cha shilingi bilioni 1.4 na baada ya Mkandarasi huyo NCL kuutelekeza Halmashauri iliamua kukamata mali zake ambazo ni magari yakutengeneza barabara.

Miradi mingine miwili iliyotembelewa na Kamati ya Bunge ni mradi wa ujenzi na ukarabat wa Shule ya Sekondari Rwazi na barabara ya rami nyepesi ya Kashai aliyopewa Mkandarasi NIKARA wa Jijini Dar es Salaam lakini miradi hiyo haikukamilika na ina mapungufu mengi na Mkandarasi aliyepewa tenda hizo hapatikani kwa mjibu wa wataalam wa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba.