Yafichuka sababu ya Kocha wa Yanga kubaki nchini


Tetesi zinaeleza kuwa kocha Mkuu wa klabu ya Yanga, Mwinyi Zahera ataondoka hii leo na ndege moja na wachezaji wa As Vita ili kuwahi katika majukumu ya timu ya taifa ya Congo ambayo tayari iko kambini tangu wiki iliyopita .

Zahera alihitajika kujiunga katika kambi hiyo Machi 13 lakini alibaki nchini kwa maagizo ya bosi wake, Kocha Mkuu wa Timu ya Taifa ya DRC, Florent Ibenge ambaye pia ni kocha mkuu wa AS Vita.

Mwinyi Zahera alibaki nchini kuufatilia mchezo wa AS Vita na Simba SC kwakuwa AS Vita ina zaidi ya wachezaji watano wanaounda kikosi cha kwanza cha DR Congo.

Kabla ya mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi kati ya Simba na AS vita Club, jana Machi 16, mashabiki wa Simba pamoja na Afisa Habari wa klabu hiyo, Haji Manara walionekana kuchukizwa na kitendo walichokiita cha usaliti ambacho kocha huyo anafanya, kwa kuahirisha safari ya kwenda Congo na kuamua kubaki na AS Vita hapa Dar es salaam.

Hali hiyo ilileta sintofahamu kwa mashabiki wa Simba ambao walikuwa wakimhofu Mwinyi Zahera kuwa kutokana na kuwafahamu vizuri Simba, angeweza kumpa bosi wake, Florent Ibenge mbinu mbalimbali za Simba.