Augua ghafla ndani ya gari na kufariki


Dickson  Archibold Maro (53) amekutwa amefariki dunia ndani ya gari IT, aina ya Noah yenye namba za cheses 603026045 baada ya kuugua ghafla.

Kamanda wa Polisi Mkoani Pwani, ACP Wankyo Nyigesa alithibitisha kutokea kwa tukio hilo, karibu na kituo cha mafuta cha state oil, huko Mdaula, Bwilingu Chalinze mkoani Pwani.

Alisema gari hiyo ilikuwa ikitokea Dar es salaam kuelekea Tunduma mkoa wa Songwe.

“Baada ya kufika kituo cha mafuta cha state oil, marehemu aliugua ghafla akiwa amepaki gari eneo hilo “alifafanua Wankyo.

Wankyo alielezea, wahudumu wa kituo hicho walitoa taarifa kwa askari polisi ambao walifika mara moja na kukuta marehemu akiwa na hali mbaya.

Jitihada za kumuwahisha marehemu kituo cha afya Chalinze zilifanyika lakini baada ya kufikishwa kituoni hapo aligundulika amesha fariki.

Hata hivyo, Kamanda huyo alisema kwamba, marehemu Dickson alipopekuliwa alikutwa na shilingi 285, 000 pamoja ,dola 400, simu mbili aina ya Itel , Tecno na karibu na gia kulikutwa  chupa mbili za maji na chupa ya juice zilizonywewa.

Wankyo alisema, utaratibu unafanyika kwa kushirikiana na clearance agency wanaohusika na upatikanaji wa bidhaa kutoka nchi moja kwenda nyingine ili liweze kuondolewa kituo cha polisi Chalinze ambapo limehifadhiwa.

Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospital ya rufaa ya Tumbi kwa uchunguzi wa daktari na ndugu wa marehemu wamejitokeza ili baada ya uchunguzi wakabidhiwe mwili huo kwaajili ya mazishi.