https://monetag.com/?ref_id=TTIb Masauni kufuatilia orodha ya vigogo wa biashara za dawa kulevya Zanzibar | Muungwana BLOG

Masauni kufuatilia orodha ya vigogo wa biashara za dawa kulevya Zanzibar


Na. Thabit Hamidu,Zanzibar

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamadi Masauni amesema yupo kufuatilia kwa karibu orodha ya majina ya wafanya biashara wakubwa wa dawa za kulevya visiwani Zanzibar.


Alisema tayari ameshakabidhiwa orodha hiyo yenye Karatasi tano inayowaonyesha wafanya biashara wakubwa wa dawa hizo.

Hayo ameyabinisha leo wakati akizungumza na Waandishi wa habari katika Ofisi za Makao makuu ya Jeshi la Polisi Zanzibar,Ziwani Mjini Magharib Unguja.

Masauni alisema anafuatilia orodha hiyo kwa kupata vielelezo vya ushahidi wa  wafanya biashara hao ili kuweza kuwashughulikia kwa kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

"Orodha hii ninayo ila nashindwa kuwataja mbele yenu wana habari kutokana na kuharibu upelelezi"Alisema Masauni.

Alisema wataendelea na kasi ya kupambana na dawa za kulevya hadi kukomesha biashara hiyo ambayo inaharibu vijana wengi Nchini.

"Tunaifanyia kazi orodha hii pia kuna wafanya biashara wakubwa wa dawa hizi wamefukuzwa bara na sasa wamekimbilia Zanzibar"alieleza Masauni.

Naibu Waziri huyo aliwataka wanzanzibar kutogopa lawama katika kusimamia vita hivyo vya dawa za kulevya na kutowachekelea kutokana na kuwa wanaiharibu Zanzibar.

Alisema bado hajaridhishwa na kasi ya mapambano ya dawa za kulevya kwa visiwani humu na kwamba katika kasi hiyo ya kupambana na dawa hizo za kulevya Tume ya Kitaifa ya Kuratibu na Kudhibiti Dawa za Kulevya Zanzibar imeelekeza malalamiko ya kuwa baadhi ya askari wa jeshi la polisi ni kikwazo.