RC Makonda aeleza kitakacho waondoa baadhi ya Watumishi Dar


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amewaweka kitimoto wakuu wa idara mbalimbali zilizopo katika halmashauri za wilaya na jiji hilo kwa kuwataka kujiandaa na uhamisho kwenda mikoani endapo idara zao zitabainika kukwamisha miradi mbalimbali.

Akizungumza katika kikao cha dharura cha Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Ilala, Makonda alisema tayari Ofisi yake imeanza kulifanyia kazi hilo ikishirikiana na Ofisi ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) kwa hatua hiyo.

Kwa mujibu wa Makonda, baadhi ya watendaji hao hususani waliokaa katika ajira zao ndani ya Jiji hilo kwa kipindi cha zaidi ya miaka kumi bila uhamisho wowote nje ya mkoa, wamekuwa kikwazo katika mikakati mbalimbali iliyo katika mpango wa maendeleo kutokana na mazoea waliyoyajenga na washika dau mbalimbali wakiwemo wakandarasi.