https://monetag.com/?ref_id=TTIb Serikali za Vijiji zazuiwa kuuza maeneo ya wazi | Muungwana BLOG

Serikali za Vijiji zazuiwa kuuza maeneo ya wazi


Serikali za vijiji mkoani Pwani zimetakiwa kutouza maeneo ya wazi yaliyotengwa kwa ajili ya uhifadhi wa mazingira ambayo hayakuhifadhiwa kisheria ili kunusuru uoto wa asili.

Aidha, viongozi hao wakiwemo watendaji watawajibika endapo kutatokea uharibifu wa mazingira kwenye misitu ambayo imehifadhiwa kisheria kwenye maeneo wanayoyaongoza.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Evarist Ndikilo aliyewakilishwa na Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Philberto Sanga kwenye kijiji cha Picha ya Ndege Vikindu wilayani Mkuranga wakati wa siku ya upandaji miti kimkoa. Ndikilo alisema kuwa serikali za vijiji zimekuwa zikiuza maeneo hayo ya wazi ambayo yamehifadhiwa kutokana na kutohifadhiwa kisheria jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

"Maeneo yaliyotengwa hayapaswi kuuzwa kwani ni maalumu kwa ajili ya kutunza mazingira na kuhifadhi uoto wa asili ambao unatoweka na kusababisha mvua kutoweka na kusababisha hali ya jangwa,"alisema Ndikilo.

 Alisema kuwa misitu iliyotengwa na ambayo haijatengwa kisheria inapaswa kulindwa na wanaopaswa kusimamia ulinzi ni viongozi kwa kushirikiana na wananchi.

"Tushirikiane kwa pamoja na wananchi ili kuhakikisha misitu inatunzwa kwani huu ndiyo uhai wetu. Tusikubali kuacha watu waiharibu kwa ajili ya kujipatia fedha," alisema Ndikilo.

 Aidha, alisema hatua zitachukuliwa kwa wenyeviti na watendaji wa vijiji endapo watashindwa kuwadhibiti watu wanaoharibu mazingira kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuchoma moto, kukata kuni, kuchana mbao, kuchoma mkaa, kujenga makazi kwenye misitu na kuharibu vyanzo vya maji.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumter Mshama, alisema kuwa lazima viongozi wa vijiji walinde mazingira ili kutopoteza uoto wa asili ambao una sababisha madhara mengi. Naye Ofisa Misitu wa Mkoa wa Pwani, Piere Ntiyamagwa, alisema kuwa katika kukabiliana na watu wanaoharibu misitu serikali kwa kushirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) wamewaondoa wavamizi 4,500.