https://monetag.com/?ref_id=TTIb Wawekezaji Wazawa watakiwa kuchangamkia fursa ya Wageni | Muungwana BLOG

Wawekezaji Wazawa watakiwa kuchangamkia fursa ya Wageni


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki amewataka wawekezaji wazawa kushirikina na wawekezaji kutoka nje ili kupata ujuzi, maarifa na kukuza mitaji na hivyo kupanua sekta ya uwekezaji nchini.

Akizungumza katika mkutano wa uwekezaji na wawekezaji kutoka Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China leo (Jumatano April 17, 2019) Jijini Dar es Salaam, Waziri Kairuki alisema kuwa wawekezaji  wazawa wanapaswa  kushirikiana na wawekezaji kutoka nje kwa kuingia ubia na makampuni ya huko ili kuchukua ujuzi katika sekta mbalimbali wazowekeza nchi.

“napenda kutoa rai kwa wawekezaji wazawa kuwa katika mikutano kama hii kwani ni fursa kwao katika kuongeza maarifa na ujuzi katika uwekezaji, na tutaendelea kukutana na wawekezaji kutoka nje ili kujua changamoto zao, lakini pia wawekezaji wazawa hatujawasahau’

Waziri Kairuki alibainisha kuwa asilimia 72 ya miradi ya uwekezaji ilioyopo nchini ni ya wazawa, ukiacha asilimia 28 ambayo ni makampuni kutoka nje na hivyo kuyataka Makampuni ya ndani kuchangamkia fursa iliyopo.

Waziri Kairuki alisema kuwa katika mkutano huo ambao ulihusisha makampuni 200 kutoka china, Taasisi zaidi ya 25 za Serikali zikiwemo TFDA, TRA, TBS na BRELA   , na Maafisa waandamizi wa Serikali za China na Tanzania, ulikuwa na lengo la kujadili na kuangalia changamoto kwa wawekezaji hao ili ziweze kutatuliwa haraka.

Aidha aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kupitia ubalozi wake hapa nchini kwa kuweza kufanikisha zoezi hilo la kuwakutanisha na wawekezaji wa China ambao wamewekeza nchini kwenye miradi mingi inayowasaidia wananchi na nchi kwa ujumla.

“Wawekezaji kutoka China wamewekeza mtaji wa dola za Kimarekani Bilioni 7, si kiasi kidogo naamini wametoa mchango mkubwa kwenye ajira, maendeleo yetu, na sekta zingine za kiuchumi hapa nchini, kwa hiyo uwekezaji huu wa miradi mingi ni fursa kwa wananchi wetu, tutaendelea kuweka mkazo kuhakikisha kuwa changamoto zinaondolewa”, alisema Waziri Kairuki.

Waziri Kairuki aliongeza kuwa katika kuchukua hatua za awali za kushughulikia changamoto kwa wawekezaji, Serikali imeondoa baadhi ya tozo mbalimbali ikiwemo tozo 114 za mazao ya kilimo zilizokuwa zikitozwa kwenye kusafirisha mazao ili kuwarahisishia wawekezaji kuwekeza nchini.

kwa upande wake Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhandisi Stella Manyanya alisema kuwa mkutano huo utafungua ukurasa mpya na fursa katika utatuzi wa changamoto kwenye sekta ya uwekezaji.

“Kupitia mkutano huu, changamoto zote za sekta ya uwekezaji zitatatuliwa, kwani uwekezaji ni sehemu ya uchumi wa nchi, kwa hiyo kwenye uwekezaji kitu kikubwa ni kujenga uelewano wa pamoja kwenye mikataba, kujenge uaminifu pamoja na utu wa kujua kwamba rasilimali zilizoko Tanzania ni kwa ajili ya” alisema Waziri Manyanya.

Naye Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt.Damas Ndumbaro alisema kuwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na China ulianza tangu ujenzi wa Reli ya TAZARA, kwa hiyo uhusiano huo utatumika kuwa kama fursa katika masuala ya uchumi.

“Tumeona Wachina wamewekeza Dola za Kimarekani bilioni 7 ndani ya Tanzania kuna makampuni 200, kwa hiyo China ni wawekezaji wakubwa hapa Tanzania, ndiyo maana katika mikutano hii tumeanza na wachina”, alisema Naibu Waziri Ndumbaro.

Kwa upande wake, Balozi wa China nchini Tanzania Wang Ke alisema  mkutano huo utaimarisha mawasiliano kati ya wawekezaji kutoka China na Tanzania kwa sababu utaleta mazungumzo mapya kwenye sekta ya uwekezaji nchini.

“Tuko hapa leo kutangaza, kuwezesha na kuhamasisha makampuni ya kutoka China kuja kuwekeza Tanzania kwenye sekta mbalimbali hasa kwenye mahoteli, kilimo na Uvuvi haya ni maeneo ya maslahi kwa uchumi wa nchi zote mbili zinazoingia katika  mikataba ya uwekezaji, na hii itaweza kuwavuta wawekezaji wengi sana kuja kuwekeza”, Balozi Wang Ke.