Waziri awaagiza Polisi kumkamata Mhandisi


Waziri wa Maji, Prof. Makame Mbarawa amemwagiza Mkuu wa Polisi Wilaya ya Maswa kumkamata na kumweka ndani kwa saa mbili Mkandarasi anayejenga Mradi wa Chujio la Maji Zanzui ili ajitafakari kutokana na kushindwa kukamilisha mradi huo kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitatu.

Waziri Mbarawa amesema baada ya kutoka rumande mkandarasi huyo wa Kampuni ya Pett Coperation anatakiwa kuandika maelezo ya kwanini amechelewesha mradi huku akimpa siku Saba kuukamilisha mradi huo na iwapo akishindwa kufanya hivyo atafukuzwa kazi na kufunguliwa mashtaka.
Waziri Mbarawa amesema mradi huo umekuwa ukisuasua kwa miaka minne sasa tangu uanze kujengwa mwaka 2015 wakati huo mkataba unaonyesha ulitakiwa kutekelezwa kwa muda wa miezi tisa tu.

Kwa upande wake Mkandarasi wa mradi huo ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Pett Coperation, Tryphone Elias amesema changamoto za kucheleweshewa hati za malipo zimepelekea kuongezea muda wa ujenzi hali iliyopelekea kupanda kwa bei ya bidhaa zinazotakiwa katika mradi huo.