Mawakili walivyowasilisha majumuisho ya mauaji ya mwanafunzi wa scolastica

Upande wa Jamhuri katika kesi ya mauaji ya mwanafunzi wa Scolastica, Humphrey Makundi umewasilisha majumuisho ya kesi hiyo na kueleza kuwa umeweza kuthibitisha shtaka dhidi ya washtakiwa wote.

Hata hivyo kwa upande wao, mawakili wa utetezi katika majumuisho yao wameeleza kuwa upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha shtaka dhidi ya washtakiwa na kuiomba mahakama iwaachie huru.

Washtakiwa katika kesi hiyo ni mlinzi wa shule hiyo, Hamis Chacha, mmiliki wa shule, Edward Shayo maarufu kwa jina la “Kingsize” na mwalimu wa nidhamu, Laban Nabiswa ambaye ni raia wa Kenya.

Hayo yamo katika majumuisho yaliyowasilishwa mahakamani kwa njia ya maandishi Ijumaa iliyopita na mawakili baada ya Jaji Firmin Matogolo anayesikiliza kesi hiyo kutaka itumike njia hiyo.

Jopo la mawakili wa Jamhuri ambao waliita mashahidi 18 na vielelezo 12 liliongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Joseph Pande akisaidiwa na Abdalah Chavulla, Omary Kibwana na Lucy Kyusa.

Katika majumuisho hayo, mawakili hao wa upande wa mashtaka walitaja hoja nne zilizotakiwa kujibiwa ambazo ni pamoja na kama mwanafunzi huyo alitoweka shuleni Scolastica Novemba 6,2017.