https://monetag.com/?ref_id=TTIb Mnada wa Ufuta waingiza Bil. 2 | Muungwana BLOG

Mnada wa Ufuta waingiza Bil. 2


Wakulima wa ufuta wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma wamepongeza serikali kwa usimamizi mzuri wa soko la zao hilo kupitia mnada uliowezesha kulipwa shilingi bilioni mbili  .

Akizungumza wakati wa mnada wa pili wa zao la ufuta uliofanyika jana  wilayani hapo, Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika  cha Songea na Namtumbo(SONAMCO), Salum Brashi  amesema,serikali imefanya uamuzi sahihi kuanzisha minada ya ufuta

“Bei ya ufuta katika mnada wa leo imeweza kupanda kutokana na wanunuzi wengi kujitokeza hapa Namtumbo hivyo kufikia kilo kuuzwa shilingi 3,061 tofauti na mnada wa kwanza kilo iliuzwa shilingi 3,010,”alisema Brashi.

Alisema haya ni mafaniko makubwa na ukombozi wa kiuchumi kwa wananchi wa Namtumbo

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mnada wa  pili wa ufuta ,Afisa Kilimo Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Enock Ndunguru alisema jumla ya makampuni 13 yalijitokeza kuomba kununua ufuta

Ndunguru alisema kwenye mnada huo jumla ya tani zilizokuwa katika ghala ni 666.26 ambapo bei ya juu iliyofikiwa na kampuni ilikuwa shilingi 3,061

Kampuni ya YIHAI Kerry  toka China ilitangazwa kushinda mnada huo kwa kununua tani 400 kwa shilingi 3,061  ikifuatiwa na  kampuni ya Export Trading ya Tanzania ikinunua tani 266.2 zilizosalia kwa shilingi 3,050 kwa kilo ya ufuta.

“Jumla ya shilingi 2,034,630,000/- zimepatikana kwenye mnada huo ambapo bei ya uwiano ni shilingi 3,055 huku mkulima akilipwa shilingi 2,774.04 kwa kilo ya ufuta na makato yote yatakuwa shilingi 281 kwa kilo “ alisema Ndunguru

Mnada wa kwanza wa ufuta katika wilaya ya Namtumbo ulifanyika wiki iliyopita ambapo jumla ya tani 240.26 zenye thamani ya shilingi 723,201,263 zilipatikana kwa bei ya shilingi 3,050 kwa kilo.

Kwenye mnada huo wa kwanza kampuni ya Sunshine Commodities Private ltd ya Mtwara ilishinda kati ya kampuni saba zilizojitokeza.