Mtanzania aibuka mshindi wa pili ‘Miss World Landscape’


Mrembo wa Tanzania, Anita Mlay ameibuka mshindi wa pili katika mashindano ya Miss World Landscapes ya dunia nyuma ya mnyange kutoka Marekani.

Katika shindano hilo lililofanyika Juni 5, 2019, Beijing, China, Anitha amemshinda mrembo kutoka Colombia aliyeshika nafasi ya tatu huku ya nne ikichukuliwa na Poland.

Anitha anayesoma stashahada ya sheria, amepeperusha vyema bendera ya Tanzania katika fainali za mashindano hayo zilizofanyika Jumatano.

Shindano hilo la urembo la kimataifa linalobeba kampeni za utunzaji mazingira, kupiga vita ujangili pamoja na kutangaza utalii limeshirikisha warembo kutoka mataifa 41.

Mratibu wa mashindano hayo nchini, Happy Maina amesema lengo kuu la kushiriki katika shindano Miss Landscape International ni kujiweka karibu na masuala ya kijamii ikiwemo utunzaji wa mazingira na kuitangaza nchi kimataifa.

"Naamini ushindi wa Anitha ni wa Taifa. Tumefurahi kuona bendera ya nchi yetu imepeperushwa hasa kwa kuona mrembo wetu ameweza kuchuana na wa Marekani mpaka hatua ya mwisho. "