https://monetag.com/?ref_id=TTIb Aggrey Morris kuwa nje ya uwanja kwa miezi miwili | Muungwana BLOG

Aggrey Morris kuwa nje ya uwanja kwa miezi miwili

Nahodha wa Klabu Azam FC, Aggrey Morris, anatarajia kuwa nje dimba kwa muda wa miezi miwili ijayo baada ya kufanyiwa upasuaji wa goti nchini Misri juzi.

Morris aliumia kwenye mchezo wa kirafiki wa timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' dhidi ya Misri wakati ikijiandaa na michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON) inayoendelea kutimua vumbi nchini Misri.

Kwa mujibu wa ripoti ya Daktari wa Azam FC, Dk. Mwanandi Mwankemwa, aliyekwenda nchini humo kushugulikia matibabu yake inaeleza kuwa, beki huyo kisiki alikuwa na uvimbe kwenye kisahani kidogo juu ya goti (patella) na kuchanika kidogo kwa mtulinga wa pembeni wa goti lake.

"Agrey amefanyiwa operesheni kuondoa uvimbe huo na kufanyiwa 'repair' kwa mtulinga wa pembeni wa goti lake na ameelekezwa mazoezi ya kufanya kwa wiki mbili, baada ya siku 14 kutoka alipofanyiwa upasuaji atatolewa nyuzi na ataanza mazoezi ya GYM moja kwa moja," ilieleza taarifa hiyo.

Mwankemwa alisema kuwa baada ya siku 21 (wiki tatu) tokea afanyiwe upasuaji, mchezaji huyo mwandamizi wa Azam FC ataanza mazoezi ya kukimbia kidogo kidogo huku akitarajia kurejea dimbani kwa ajili ya ushindani baada ya siku 60 kupita.

Beki huyo amekuwa nguzo muhimu ya ulinzi tokea kujiunga na Azam FC mwaka 2009 akitokea Mafunzo ya Zanzibar, msimu uliopita akiiongoza timu hiyo kutwaa mataji matatu, Kombe la Kagame, Mapinduzi na la Shirikisho la Azam Sports.