Fahamu namna ya kupatwa kwa mwezi na athari zake



Shirika la maswala ya angani dunini NASA linasema kuwa hakuna ushahidi unaounga mkono wazo kwamba kupatwa kwa mwezi kuna athari za moja kwa moja miongoni mwa binadamu.

Lakini linakiri kwamba tukio hilpo linaweza kutoa athari za kisaikolojia ambazo zinaweza kuathiri maungo kutokana na imani za watu na hatua wanazochukua kutokana na imani hizo.

Kupatwa kwa mwezi hutokea wakati mwezi unapopita katika kivuli cha dunia ukiwa mbali na jua. Kupatwa kwa mwezi husababisha kupotea kwa mwangaza ndani yake.

Mwezi kwanza huingia katika kivuli cha dunia polepole hatua inayoitwa penumbra kwa lugha ya kiingereza.

Mwanga wa mwezi hupungua polepole na kuonekana kuwa na giza linaloelekea kutoka kulia likienda kushoto na kusababisha kupatwa kamili kwa mwezi.

Wakati mwezi unapoingia katika kivulivuli cha dunia chenye giza totoro, unaonekana kana kwamba umeliwa kidogo. Kipande hicho kilicholiwa kinaendelea kupanuka hadi mwezi wote unapopatwa kamili.

Baadaye huonekana kama ulio na rangi ya machungwa iliochanganywa na nyekundu.

Wakati mwezi unapoondoka katika kivuli hicho cha dunia hali ya kawaida ya mwezi huo huanza kurejea.

Kupatwa kwa mwezi huchukua muda wa saa tatu ili kukamilika.

Kwa jumla muda unaochukuliwa na mwezi unapopatwa kamili ni saa moja huku muda huo ukitofautiana kila mwezi unapopatwa.

Mvutano uliopo katikati ya jua na mwezi husababisha maji kuongezeka baharini kila Jua mwezi na dunia zinapokuwa katika mstari mmoja.

Kwa kuwa kupatwa kwa mwezi hufanyika wakati wa mwezi mkubwa mawimbi baharini huwa makubwa wakati wote.

Hapo zamani watu walikuwa wakiamini kwamba wanyama pori hubadilisha tabia zao wakati wa kupatwa kwa mwezi .

Utafiti wa tumbiri uliofanywa na chuo kikuu cha Pennsylvania nchini Marekani ulionyesha kuwa kubadilika kwa tabia za wanyama hao wakati wa tukio hilo.

Utafiti huo unasema kuwa mabadiliko hayo ya tabia hutokana na kupungua kwa mwangaza wakati wa kupatwa kwa mwezi.

Huku sayansi ikikosa kupata athari zozote za kupatwa kwa mwezi miongoni mwa binadamu, imani kuhusu kupatwa kwa mwezi na athari zake imesababisha mabadiliko miongoni mwa binadamu katika historia yao.

Kupatwa kwa mwezi huonekana kama ishara za kitu kibaya ama swala linalohusishwa na bahati mbaya hivyobasi watu hujitolea kutoa sadaka kwa kuchinja wanyama ili kuondoa ile inayosemekana kuwa hasira ya mungu.